Mwameja awataka wachezaji Ligi Kuu Tanzania kujituma

Muktasari:

Imeelezwa Ligi Kuu Tanzania Bara (VPL) imeanza kwa ushindani msimu huu, wachezaji wameshauriwa kujituma na kuacha kulewa sifa.
 

Dar es Salaam.Kipa wa zamani wa Simba, Mohamed Mwameja amesema kama wachezaji watajituma kwa bidii anaamini Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara (VPL) itakuwa bora zaidi.

Mwameja amesema ligi ya VPL imeanza kwa ushindani wa hali ya juu, anachoshauri ni wachezaji kujitoa kwa timu walizoajiriwa nazo ili kufanya vitu vikubwa.

Alisema anaona vipaji vikubwa katika ligi hiyo, isipokuwa wasiwasi wake ni kwa wachezaji kujisahau na sifa ambazo wanakuwa wanazipata kutoka kwa mashabiki wao.

"Kila mchezaji akiwa anajitambua kwa nini yupo kwenye timu aliopo bila shaka kunaweza kukapatikana ushindani utakaofanya ligi ikawa na mvuto,"

"Ushindani unapokuwa mzuri ndivyo timu yetu ya taifa inapokuwa na kikosi kizuri, wachezaji wajitolee watafanya makubwa na kufika mbali zaidi hata wao wenyewe," alisema Mwameja.