Mkwasa akomalia ushambuliaji Yanga ikijianda kuivaa Alliance

Muktasari:

Yanga kesho watakuwa wageni wa Alliance FC katika mchezo utakaochezwa kwenye Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza.

Mwanza. Kocha wa Yanga, Charles Mkwasa alitumia muda mwingi wa mazoezi ya leo jioni kuwasuka washambuliaji wake namna ya kufunga.

Yanga kesho watakuwa wageni wa Alliance FC katika mchezo utakaochezwa kwenye Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza.

Katika mazoezi hayo Mkwasa amewataka wachezaji wake kushambulia kupitia pembeni huku washambuliaji wa kati akiwataka kuingia kwa kasi sana katika eneo la 18 kumalizia krosi hizo cha chinichini.

Mara nyingi wachezaji huwa wanagawanywa kwa makundi kutokana na idara zao, hii leo mabeki kama Ally Mtoni wamekomaliwa nao kucheza kwa kushambulia zaidi.

 

 

Baada ya kumaliza mazoezi hayo ya kushambulia kwa ushirikiano, Mkwasa aliwataka wachezaji wake kupiga mipira mirefu nje ya 18 wakimjaribu kipa Ramadhani Kabwili.

Naye Kocha Msadizi wa Yanga, Said Maulid 'SMG' amesema hali ya hewa ya Mwanza sio mbaya hivyo wapo sawa kuelekea katika mchezo huo japokuwa anajua wazi kuwa utakuwa mgumu kwa sababu Alliance wametoka kupoteza mechi yao ya mwisho dhidi ya Azam.

"Hatuangalii sana idadi ya mabao, sisi tunaangalia zaidi pointi tatu tu, morali ya wachezaji ipo juu nadhani umewaona walivyo changamka mazoezini, tunatarajia kushinda" alisema SMG.

SMG alisema mapungufu yaliyokuwepo kwenye safu yao ya ulinzi tayari wameyafanyia kazi hivyo kuelekea katika mechi hiyo ya muhimu kwa pande zote hawana wasiwasi wowote.