Bondia Mfaume, Keis wataka kuzichapa kavu kavu

Muktasari:

Mzazi anayemnoa Keis anatokea kambi ya Manzese na amewahi kunolewa na Rama Jaha ambaye ni kocha wa Mfaume, lakini wakaibua bifu baada ya kila mmoja kujitangazia ufalme wa ndondi katika maeneo hayo.

Dar es Salaam.Mabondia Mfaume Mfaume na Ally Keis nusura wazichape kavu kavu wakati wa kutambulisha pambano lao la utangulizi litakalopigwa Novemba 29 kuwasindikiza Hassan Mwakinyo na Arnel Tinampay.

Mfaume na Keis wanatoka kambi ya Manzese na Mabibo watacheza pambano la utangulizi la raundi 10 kwenye uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam.

Wakati wa kutambulishwa, Keis alimtambia Mfaume akidai ni bondia wa kawaida kwake, hampi presha na hamhofii kwa chochote, wakati akitamka hayo, mamia ya mashabiki waliokuwa wakimshangilia Mfaume walimzomea wakimkebehi kuwa njaa ndio zimempeleka kucheza pambano hilo, lakini hamuwezi Mfaume.

Hata hivyo Mfaume alivyoitwa ulingoni, alionekana kupaniki na kabla ya kupanda alimuita mpinzani wake huyo chini ya ulingo ili wazichape, lakini Keis aliendelea kumkebehi akidai bondia huyo ameingia kwenye 18 zake.

Baada ya kauli hiyo, Mfaume alimvamia Keis na kutaka kuzichapa kabla ya kuzuiwa na mabaunsa huku mpinzani wake akijibu mapigo kabla ya makocha wao, Rama Jaha na Christopher Mzazi kutakiwa washikane mikono wakiambiwa ngumi si vita.