Mwana FA atoka na ‘Gwiji’

Muktasari:

Mwana Fa ni miongoni mwa wasanii waliodumu kwa muda mrefu akitamba na nyimbo zake kama Mimi na Mabinti, Yalaiti, Natamani.

BAADA ya kimya kirefu msanii wa mziki wa Hip Hop nchini, Mwana FA ameachia wimbo wake mpya unaoitwa Gwiji.

Wimbo huo unatoka baada ya kupita miezi 10 tangu alipoachia wimbo wake wa 'Endelea tu' na kufanya vizuri kwa kutazamwa na watazamaji Milioni moja katika mtandao wa You Tube.

Mwana FA aliachia wimbo wa Gwiji jana Jumatano na mapokezi yake yamekuwa makubwa hususani katika mitandao ya kijamii tangu wimbo ulipotoka.

Katika mtandao wake wa You Tube, licha ya kupita saa 14 tangu wimbo huo uachiwe, tayari umetazamwa mara Elfu 64 huku ukiwa unaendelea kutazamwa kila dakika.

Mashairi ya kwenye wimbo huo yameelezea namna ambavyo mwanaume anapambana kuhakikisha kwamba maisha yake yanaenda sawa.

Sehemu ya mstari mmoja inasema "Tushasukuma sana milango iliyoandikwa vuta, na ikafunguka", hii ina maanisha kabisa kwamba kuna muda inabidi ufosi katika unachokiamini.

Mwana FA amekuwa ni msanii ambaye anatunga mashairi yanayozungumzia jamii zaidi na kugusa katika kila rika.