VIDEO: Mwakyembe atoa fufafanuzi fedha za Magufuli

Muktasari:

Waziri Mwakyembe amesema kwa sasa sio jambo zuri kuendelea kujadili suala la fedha zilizotolewa na Rais Magufuli kwakuwa lipo Takukuru na linafanyiwa kazi.

Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dk. Harrison Mwakyembe amesema mjadala kuhusu fedha zilizotolewa na Rais Magufuli kwa ajili ya maandalizi ya Fainali za Mataifa ya Afrika kwa Vijana chini ya umri wa miaka 17 (Afcon U17) yaliyofanyika nchini mwaka jana usitishwe kwa sasa kwa vile lipo katika vyombo husika.

Kauli hiyo ya Waziri Mwakyembe imekuja siku mbili baada ya Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) kuanza kuwahoji baadhi ya watu juu ya matumizi mabaya ya fedha kiasi cha zaidi ya Sh 1 bilioni ambazo zilichangwa na Rais Magufuli na baadhi ya taasisi ili kufanikiha mashindano hayo.

"Nmefurahi sana kwasababu Takukuru wanaliangalia hili suala, kwa sababu hiki chombo tulikiunda sisi wenyewe, na kwenye wengi pana mengi.

"Pesa tuliyopokea ni nyingi sio hiyo tu, wengi mnaongelea Shiling 1Bilioni lakini bajeti yetu ilikuwa zaidi ya  Sh 3 Bilioni, hivyo tuwaache Takukuru wachunguze zaidi na watakaokutwa wamefanya makosa watawajibika," anasema Mwakyembe.

Kuhusu kurejea kwa ligi amesema moja ya vitu ambavyo anavitambua ni suala la uchumi kwa timu zetu.

"Ule utaratibu wa zamani, timu inatoka Songea kwenda Mara na Mara kwenda Mtwara hawataweza lazima tulitambue kwa sababu wamesimama na hawana kipato na wamelipa wachezaji.

"Pili nikaomba kwasababu ni viporo tu ndivyo vimebaki hivyo tusiingie na yale makandokando ya nyuma kwa mfano marefa hawalipi hili ni jambo ambalo silifurahii," alisema Mwakyembe.

Kuhusu idadi ya wachezaji wa kigeni anasema BMT wanaendelea kuliratibu na linaendelea vizuri.

"Watanzania hawajui kujadili kwa hoja asilimia 90 kwenye mitandao ya kijamii ni matusi, wao wanadhani serikali inaomba ruhusa. Serikali ya awamu ya tano inapenda kuwahusisha watu.

"Sisi kama serikali tunaweza kuamua muda wowote na hakuna wa kutuambia kitu maana vibali vyote vinatoka serikalini.

Leo Ijumaa Serikali pamoja na uongozi wa Bodi ya Ligi na TFF walitarajia kukutana na kujua namna ya kumalizia michezo ya ligi mbalimbali lakini hakikufanyika na kinatarajia kufanyika kesho kutokana na sababu ambazo hazikuwekwa bayana.