Mwakinyo amzidi uzito Mfilipino Tinampay kuzichapa kesho

Muktasari:

Baada ya Mwakinyo kushuka katika mzani na kuonekana amezidi kilo, mpinzani wake Mfilipino aliambiwa na kuonyesha wasiwasi hivyo kutaka wapime tena.

Dar es Salaam. Mabondia Hassan Mwakinyo amemzidi kilo 1 mpinzani wake Arnel Tinampay atakayepambana naye katika uzani wa Super Welter kesho kwenye Uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam.

Katika tukio la kupima uzito huo Mwakinyo alikuwa na kilo 70.6 wakati Tinampay alikuwa na kilo 69.7, pia mabondia hao walipimaji wa afya zao chini ya madaktari kutoka hospital tatu za Temeke, Sanitas na Sali International.

Baada ya Mwakinyo kushuka katika mzani na kuonekana amezidi kilo, mpinzani wake Mfilipino aliambiwa na kuonyesha wasiwasi hivyo kutaka wapime tena.

Hata hivyo walipopima tena bado uzito ulisoma vile vile ndipo Mfilipino alipoulizwa je anakubali kupigana na mpinzani wake ambaye amemzidi uzito na yeye kukubali.

Mwakinyo amesema wakati akiwa Tanga uzito wake ulikuwa sawa na mpinzani wake, lakini kutoka na kupata vimiminika wakati alitoka Tanga kuja Dar es Salaam inawezekana ikawa sababu mojawapo ya kilo zake kuongezeka

"Sikuona sababu ya yeye kuwa na wasiwasi kwani huwa inatokea mnaweza mkakutana mabondia mnazidia kilo hata mbili, lakini mkawa mpo katika uzani mmoja.

"Nilikiwa na kilo sawa wakati nipo kambini Tanga, lakini wakati niko safari kuja Dar es Salaam nilikuwa napata kimiminika juisi nahisi inaweza kuwa sababu," alisema Mwakinyo.