Mudathir: Uchovu kikwazo cha Azam mbio za ubingwa

Muktasari:

  • Azam FC wametua jijini Dar es Salaam leo wakitokea Zanzibar walikotwaa ubingwa wa Mapinduzi wameahidi kupambana na kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu Bara na Kombe la FA.

Dar es Salaam. Kiungo wa Azam FC, Mudathir Yahya amesema pamoja na kufanikiwa kutwaa ubingwa wa Kombe la Mapinduzi bado watakuwa na wakati mgumu zaidi kutunza viwango vyao kutokana na kucheza michezo mfululizo.

Azam imefanikiwa kutwaa ubingwa wa Mapinduzi baada ya kuifunga Simba 2-1 na wamerudi jijini Dar es Salaam tayari kwaajili ya kuendelea na Ligi Kuu Bara.

Akizungumza Dar es Salaam leo muda mchache baada ya kutua uwanja wa ndege wakitokea Zanzibar, Yahya alisema mashindano hayo yanafaida na hasara kwao kutokana na ushindani wa ligi.

Alisema wamefurahi kutwaa ubingwa wa mapinduzi, lakini wanatarajia kukutana na changamoto ya uchovu katika ligi kutokana na kucheza michezo mfululizo wakiwa visiwani bila ya mapumziko.

"Tunafuraha ya kutwaa ubingwa ikiwa ni mara tatu mfululizo, lakini pamoja na ushindi huo bado tutakuwa na changamoto ya uchovu katika ligi ambayo tunatarajia kuanza Jumanne kwa kumenyana na Ruvu Shooting," alisema kiungo huyo.