Mtibwa yaiendea KCCA Sobibo

Muktasari:

  • Mtibwa Sugar wanatarajiwa kutua leo Alhamisi jijini Dar es Salaam baada ya kufanikiwa kuvuka hatua inayofuata ya mashindano ya Kombe la Shirikisho  Kutokana na kuing'oa Northen Dyamo ya Shelisheli kwa jumla ya mabao 5-0.

UPO uwezekano mkubwa kwa wawakilishi wa Tanzania, Mtibwa Sugar kwenda kuwafanyia maandalizi KCCA mkoani Kagera katika kambi ya Kagera Sugar maarufu kwa jina la Sobibo.

Mtibwa Sugar ambayo imefuzu hatua ya awali baada ya kuing’oa Northen Dyamo ya Shelisheli kwa jumla ya mabao 5-0, sasa inajiandaa na mechi za raundi ya kwanza dhidi ya KCCA ya Uganda.

Kikosi hicho ambacho maskani yako ni Mtibwa katika mji wa Mabao mkoani Morogoro, kimepanga kwenda kujificha Kagera kwa ndugu zao hao Kagera Sugar.

Hii ni kutokana na utulivu uliopo katika kambi hiyo iliyopo maeneo ya Missenyi na sababu ya kupewa jina la Sobibo ni utulivu na ugumu wakiifananisha na ile ya wapiganaji wa Nazi ya Sobibo.

Mtibwa ilitarajiwa kuwasili nchini jana Jumatano kwa ndege ya Emirates wakipitia Dubai. Inatarajia kucheza mechi ya raundi ya kwanza kati ya Desemba 14-15, nchini Uganda na wa marudiano ni Desemba 23-24, jijini Dar es Salaam.