Mtanzania kuzichapa pambano la AJ vs Andy Ruiz

Muktasari:

Swedi atapanda ulingoni akiwa na rekodi ya kucheza mapambano 20, ameshinda 12, amepigwa mara sita na kutoka sare mapambano mawili.

BONDIA Mtanzania Swed Mohammed ni miongoni mwa watakaozichapa mapambano ya utangulizi kuwasindikiza Anthony Joshua (AJ) na Andy Ruiz Jr nchini Saudi Arabia.

AJ na Ruiz Jr  watazichapa pambano la marudiano litakalopigwa Ukumbi wa Diriyah Arena mjini Diriyah Desemba 7.

Katika pambano hilo ambalo litafuatiliwa na maelfu ya mashabiki wa ngumi duniani, Mohammed atazichapa pambano la utangulizi kuwasindikiza wababe hao wa ngumi wa uzani wa juu wa dunia.

Mtanzania huyo ambaye jina lake la utani ni Nuclear atazichapa na  Ivan 'Hopey' Price pambano la uzani wa bantam kilo 56 dakika chache kabla ya AJ na Andy Ruiz Jr kupanda ulingoni kumaliza ubishi wa nani mkali.

Mabondia hao watawania mataji ya dunia ya WBA, IBF, WBO na UBO ambayo Andy Ruiz Jr ambaye ni bondia namba moja wa dunia kwenye uzani wa juu atakuwa akiyatetea baada ya kumchapa kwa TKO, Joshua aliyekuwa akiyashikilia na kumshusha kutoka kuwa bondia wa dunia kwenye uzani huo.