VIDEO: Msuva: Mechi na Cape Verde Watanzania msihadithiwe!

Muktasari:

  • Kuelekea mchezo wa Taifa Stars na Cape Verde winga wa Tanzania, Simon Msuva amesema, mchezo huo si wa kukosa kabisa kuungalia na watapata matokeo mazuri tu.

Cape Verde. Winga wa Timu ya Taifa Stars, Simon Msuva amewaambia Watanzania mchezo wao dhidi ya Cape Verde si wa kukosa kabisa kuuangalia kwa sababu utakuwa wa aina yake.

Msuva ambaye aliungana na kikosi cha Taifa Stars nchini humo akitokea  Morocco pamoja na nahodha wa timu Mbwana Samatta anayekipiga klabu ya Genk ya nchini Ubelgiji.

Amesema, wamefanya maandalizi ya kutosha na hivyo, kazi iliyobaki ni maombi tu kutoka kwa Watanzania.

"Ni mchezo ambao Watanzania wengi wanatakiwa kuiangalia kwani kwa imani yangu kuna kitu kizuri kutoka kwetu lakini pia watuombee ili tufanye vizuri zaidi,"alisema Msuva.

Amesema, katika mbinu, ufundi na utimamu wa akili watakavyo ucheza mchezo huo ambao utapigwa majira ya saa 2:00 usiku kwa masaa ya Tanzania, hautakuwa tofauti sana na ule wa Uganda.

"Kwa sababu tutakuwa ugenini, hatutaweza kucheza tukishambulia muda wote, lazima tutafanya mashambulizi ya kushtukiza na kuzuia zaidi,"alifafanua Msuva ambaye anakipiga klabu ya Difaa el Jadida.       

Amesema, licha ya kuwa watacheza kwenye uwanja wa nyasi bandia ambao ni tofauti na wa Taifa kwao hawana wasiwasi.