Mkwasa aendeleza ushindi Yanga

KAIMU Kocha Mkuu wa Yanga, Boniface Mkwasa 'Master' ameendelea kuchekelea kibarua chake cha muda baada ya leo Ijumaa timu yake kuibuka na ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Alliance FC .
Katika mchezo huo uliopigwa Uwanja wa CCM Kirumba jijini hapa, Yanga walikuwa wa kwanza kufumania nyavu za Alliance kupitia mshambuliaji wao Patrick Sibomana dakika ya 25 ya mtanange huo.
Kipindi cha pili kilianza kwa kasi ambapo Alliance FC walicharuka na kuanza kulisakama lango la Yanga na kusawazisha bao hilo dakika ya 54 kwa shuti kali la kiungo mkabaji, Juma Nyangi.
Licha ya kusawazisha bao hilo, Alliance walijikuta wananyukwa bao la pili kupitia David Molinga dakika ya 71 ya mchezo ambalo lilizamisha kabisa Jahazi lao na kupelekea wapoteze mchezo huo wakiwa nyumbani.
Mkwasa amekuwa na mwendelezo mzuri wa matokeo tangu alipopewa kibarua hicho cha kuinoa Yanga baada ya Mwinyi Zahera kutimuliwa, katika mechi tatu ambazo Mkwasa ameongoza ambapo ameshinda zote.