Mkwasa : Tungezubaa tu Alliance wangetupiga

Muktasari:

Alisema kama wasingekomaa basi mchezo huo ungekuwa mgumu kwao kwani Alliance walipata upinzani mkubwa ambao aliujua tangu wanaingia Mwanza kwamba wanapaswa kupambana zaidi.

KOCHA wa Yanga, Boniface Mkwasa amekiangalia kikosi cha Alliance FC ndani ya dakika 90 walizocheza nao kisha kutamka wazi kuwa kama wangewachekea basi  wangefungwa.
Yanga kwa mara ya nne  juzi Ijumaa iliwatandika Alliance mabao 2-1 katika mchezo wa Ligi Kuu Bara uliopigwa uwanja wa CCM Kirumba jijini hapa.
Mkwasa alisema waliingia kwa tahadhari kubwa katika mchezo huo kitu ambacho kiliwasaidia kupata ushindi kwani walijua Alliance ni timu nzuri na ina wachezaji wenye vipaji.
Alisema kama wasingekomaa basi mchezo huo ungekuwa mgumu kwao kwani Alliance walipata upinzani mkubwa ambao aliujua tangu wanaingia Mwanza kwamba wanapaswa kupambana zaidi.
"Nilijua tangu tumekuja hapa Mwanza kuwa tusiende kucheza kwa kuwadharau Alliance na kweli umeona walivyotupa upinzani na tusingekomaa mambo yangekuwa magumu sana kwetu," alisema Mkwasa.
Alisema Alliance ni bonge la timu na kama wakiendelea hivyo watakuwa tishio kwenye ligi maana wanacheza soka safi na lenye nidhamu kubwa uwanjani.
"Ni timu nzuri sana kwangu naona watafika mbali sana Alliance ina wachezaji ambao kama wakiendelezwa vyema basi watakuja kuwa nyota wakubwa hapa Bongo"alisema Mkwasa.