Mkude, Juuko wakacha mazoezi Simba

Muktasari:

Beki Juuko naye hakusafiri na timu kwenda Algeria kwa kuwa na kadi, pia alikosa mechi za Ligi Kuu Bara dhidi ya Lipuli na Stand United kwa kuwa ni majeruhi.

Dar es Salaam. Kiungo mkabaji wa Simba, Jonas Mkude na beki Juuko Murshid hawakutokea katika mazoezi ya timu hiyo yaliyofanyika leo kwenye Uwanja wa Boko Veteran, Dar es Salaam.

Mkude anatumikia adhabu ya kadi tatu za njano hivyo hataweza kucheza mechi ya mwisho ya Simba dhidi ya AS Vita.

Beki Juuko naye hakusafiri na timu kwenda Algeria kwa kuwa na kadi, pia alikosa mechi za Ligi Kuu Bara dhidi ya Lipuli na Stand United kwa kuwa ni majeruhi.

Juuko alikosa mechi hizo kwani alikuwa akisumbuliwa na maumivu aliyoyapata katika mechi dhidi ya Al Ahly.

Habari njema kwa Simba ni kurejea mazoezi kwa beki wake Erasto Nyoni aliyekuwa majeruhi pamoja na mshambuliaji Emmanuel Okwi wote walikosa mechi iliyopita ya Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya JS Saoura.

Katika mazoezi ya leo Alhamisi Nyoni, Okwi walionekana kuwa fiti na kufanya mazoezi yote ya nguvu waliyofanya wachezaji wengine.

Kulingana na mazoezi yalivyo na Nyoni alivyofanya vizuri huenda akaanza katika kikosi cha kwanza kwenye mechi na AS Vita.