Mkude, Juuko kuwakosa AS Vita, Nyoni ndani...

Muktasari:

Simba na AS Vita wanacheza mechi ya Ligi ya Mabingwa Afrika hatua ya makundi kwa Kundi D. Mchezo huo ni wa mwisho na mshindi ataingia robo fainali.

Dar es Salaam. Beki wa kati wa Simba na timu ya Taifa ya Uganda 'The Cranes', Juuko Murshid, kiungo Jonasi Mkude pamoja na Shomari Kapombe wataukosa mchezo wao wa kesho Jumamosi dhidi ya AS Vita unaotarajiwa kupigwa saa 1:00 jioni,  Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.

Mchezo huo ambao ni wa Ligi ya Mabingwa Afrika hatua ya makundi, kila wachezaji ana matatizo tofauti lakini habari njema ni kwamba, kiraka Erasto Nyoni aliyekuwa majeruhi kwa muda mrefu na Emmanuel Okwi aliyekosa mchezo uliopita na JS Saoura nchini Algeria, wanaweza kuwepo katika kikosi kitakachoanza kesho dhidi ya AS Vita.


Kocha Mkuu wa Simba, Patrick Ausems amesema, Mkude atakosekana katika mchezo huo kwa sababu anatumikia adhabu yake ya kadi tatu za njano.

Amesema mabeki wake, Juuko na Kapombe hawako vizuri kiafya lakini Erasto Nyoni na Okwi wameimarika na upo uwezekano wa kucheza.


"Wachezaji hao watatu hawatakuwa sehemu ya mchezo wetu na AS Vita. Kila mmoja anatambua umuhimu na uwezo wa wachezaji hao lakini hakuna namna nyingine ya kufanya,"anasema Aussems ambaye kama kesho wataibuka na ushindi wataweka historia ya kutinga hatua ya robo fainali ya michuano hiyo.


Amesema pamoja na kuwakosa wachezaji hao si kigezo cha wao kushindwa kupata matokeo mazuri mbele ya AS Vita.