Mke wa Tambwe ajipa jukumu zito

Muktasari:

Mshambuliaji Amissi Tambwe tangu atoke kwenye maumivu ya mguu katika msimu huu wa ligi ameshafunga mabao manne kwenye msimamo wa wafungaji bora ambao kinara ni Eliud Ambokile wa Mbeya City mwenye tisa.

MKE wa straika wa Yanga, Mrundi Amissi Tambwe amesema, anaendelea kuifanya kazi yake kama mama kuhakikisha mumewe anakuwa tishio zaidi kama zamani na kiu yake ni kumuona kileleni mwa orodha ya Wafungaji Bora wa Ligi Kuu Bara.
Raiyan Mohammed 'Ray wa Tambwe', alisema kama mke anatambua wajibu wake mkubwa ni kuhakikisha Tambwe anakuwa mkali kwa kumsaidia kwa hali na mali.
"Kazi yangu ni kutunza familia, watoto na mume wangu kwani wanapofanikiwa wao ni mafanikio yetu sote. Licha ya Tambwe kuanza kufanya vizuri uwanjani kwangu bado kabisa nataka kumwona hivyo katika mechi nyingi zijazo," alisema Raiyan aliyedai bado Tambwe hajarejea kwa asilimia zote kama enzi zake.
Kutokana na hilo ndiyo maana anakazia kuwa hata kwa upande wake kama mke bado ana kazi kubwa ya kufanya ili asimame juu kileleni.
"Maneno mazuri, kumfariji na kumtia moyo kwenye kazi yake atakaa vizuri tu, mambo taratibu kwa sababu nafahamu anajua na kilichokuwa ni changamoto za hapa na pale," alisisitiza Raiyan aliyefunga ndoa na Tambwe mwezu uliopita.
Tambwe aliyetua nchini na kujiunga na Simba katikati ya msimu wa 2012-2013, akitokea Vital O ya Burundi aliwahi kuwa Mfungaji Bora misimu miwili tofauti akiwa na klabu za Simba na Yanga kabla ya msimu uliopita kupotea kabisa kwa sababu ya majeraha na hadi sasa ametupia nyavuni mabao manne.