Mipango ya Pep msimu ujao usipime kabisa

Muktasari:

Nyota wa Leicester City, Harry Maguire ni mmoja kati ya wachezaji ambao wapo katika rada yake.

MANCHESTER,England.MANCHESTER City ndio mabingwa wa Ligi Kuu England, hili kila mtu analifahamu! Sasa habari mpya ni kwamba, licha ya kupata ubingwa, kocha wa kikosi hicho Pep Guardiola, ambaye huwa hakaukiwi kiu ya kupata ubingwa ameibuka na kusema anataka kuendelea kukisuka kikosi chake kwa ajili ya kuibuka kwa kishindo msimu ujao.

Taarifa njema kwa wapenzi wa klabu hiyo ni kuwa, Mhispaniola huyu atakabidhiwa Pauni 200 milioni kwa ajili ya kusajili nyota wa maana msimu unaokuja na tayari Guardiona ameelezea maeneo ambayo anadhani ni lazima yaboreshwe ili kuendelea kutesa msimu wa ligi ujao.

Habari zilizopo ni, kocha huyo anataka kuongeza beki mmoja, viungo wawili na mshambuliaji mmoja.

Guardiola ambaye pia anatarajiwa kupambana na Watford katika fainali ya FA wikiendi hii ameanika mpango wa kutafuta wachezaji wa kuongeza unapaswa kufanyika kwa umakini mkubwa.

Huku nahodha Vincent Kompany akiwa bado hajakubali mkataba mpya, pia Nicolas Otamendi na Eliaquim Mangala wakitaka kuondoka, mtazamo wa Guardiola upo kwa beki wa kati.

Nyota wa Leicester City, Harry Maguire ni mmoja kati ya wachezaji ambao wapo katika rada yake.

Pia, De Ligt inadaiwa kuwa karibu kwenda kukipiga huko Barcelona hivyo Manchester City wanatoa macho kwa ajili ya mchezaji wa nafasi yake. Hata hivyo, kuna mastaa wengine kibao.