Mexime: Tutawapiga JKT Tz kwao

Muktasari:

Maxime alisema wanashuka uwanjani kwa umakini na tahadhari kuhakikisha wanashinda ili kupoza machungu waliyopata kwenye mechi iliyopita na kujiweka pazuri kwenye msimamo wa Ligi Kuu.

BAADA ya kupoteza mchezo uliopita dhidi ya Simba, Kocha Mkuu wa Kagera Sugar, Mecky Maxime amesema wanajipanga kuangusha kipigo kwa maafande wa JKT Tanzania kuhakikisha wanashinda.

Kagera Sugar inawafuata Maafande hao ikikumbuka kipigo cha bao 1-0 dhidi ya vinara wa Ligi Kuu, ambapo kesho Jumamosi itakuwa ugenini kuwavaa wapinzani hao mchezo utakaopigwa uwanja wa Jamhuri jijini Dodoma.

Timu hiyo ya mjini Bukoba itakuwa na kazi ngumu kulipa kisasi kwa JKT  Tanzania, kwani katika mchezo wa raundi ya kwanza wakiwa nyumbani walilala bao 1-0.

Hadi sasa Kagera Sugar wako nafasi ya sita wakiwa na pointi 37 huku JKT Tanzania wana alama 35 wanashika nafasi ya sita baada ya timu zote kushuka uwanjani mara 23.

Maxime alisema wanashuka uwanjani kwa umakini na tahadhari kuhakikisha wanashinda ili kupoza machungu waliyopata kwenye mechi iliyopita na kujiweka pazuri kwenye msimamo wa Ligi Kuu.

“Ligi ndivyo ilivyo leo unashinda kesho unafungwa, lakini tumejipanga kupata pointi tatu dhidi ya JKT Tanzania, tunafahamu wapinzani walivyo na ushindani kwani walitufunga tukiwa nyumbani hivyo tunaenda kulipiza kwao” alisema Maxime.