Messi vs Ronaldo : Messi, baba yake kortini kwa kukwepa kodi

Muktasari:

Kutengana kule na familia kulimfanya kulisababisha Messi apitie katika kipindi kigumu lakini kuwa karibu na Jorge (baba yake) walau kulirahisisha mambo na kuonekana rahisi kwa Messi.

KATIKA toleo lililopita, mwandishi, Luca Caioli alielezea namna hali ilivyokuwa kwa Messi katika siku zake za mwanzo mwanzo Barcelona alivyopata tabu kuendana na maisha mapya ikiwamo mdogo wake wa kike aliyefuatana naye, Maria Sol kushindwa kuendana na maisha hayo. Sasa endelea…

Mbali na majanga hayo, Messi na familia yake walijikuta walikabiliana na changamoto nyingine japo mambo hayakuwa magumu sana kwa Messi ila mdogo wake wa kike, Maria Sol alikuwa na wakati mgumu kuendana na maisha mapya.

Hali hiyo iliifanya familia kuchukua uamuzi mgumu wa kuondoka miezi mitano baada ya kuwasili, mama wa Messi, Celia alilazimika kurudi Argentina na Maria Sol wakati Jorge alibaki Barcelona na watoto wa kiume.

Mambo yalikuwa magumu kwa Messi, hiyo ni sambamba na ukweli kwamba pia alikuwa akipata wakati mgumu kuwa pamoja na wachezaji wenzake kutokana na hulka yake ya kuwa mwenye kuona aibu.

“Nilijua kwamba alikuwa mbali na nyumbani, mbali na familia yake na anaishi hapa na baba yake,” anakumbushia Alex Garcia, mmoja wa makocha wa Messi wa mwanzo mwanzo Barcelona.

Kutengana kule na familia kulimfanya kulisababisha Messi apitie katika kipindi kigumu lakini kuwa karibu na Jorge (baba yake) walau kulirahisisha mambo na kuonekana rahisi kwa Messi.

“Tulitumia muda mwingi pamoja, tukawa marafiki ingawa tulikuwa na mambo yetu ya hapa na pale,” anasema Messi.

Kwa Jorge ilikuwa ni mabadiliko kutoka kuwa mfanyakazi mwajiriwa hadi kuwa meneja ilikuwa ni kama vile amekuwa na umeneja katika kinachoitwa Usimamizi wa Leo Messi.

“Haikuwa rahisi, nililazimika kujifunza, nilikuwa nayatazama mambo kwa mapana yake, nilikuwa nalazimika kumlinda kwa faida yake ya siku zijazo kutoka kwa watu waliokuwa na matarajio kutoka kwake ambao wangeweza kumharibu,’’ alisema Jorge.

Hata hivyo ni kama vile yeye mwenyewe Jorge alishindwa kumlinda mwanaye. Jorge ndiye aliyekuwa na majukumu ya kusimamia masuala ya fedha ya mwanaye na mamlaka za mapato Hispania zilijiaminisha kwamba kulikuwa na tatizo mahala, mambo hayakuwa yakienda kama taratibu zinavyotaka.

Mwaka 2013 mwendesha mashtaka wa umma, alitangaza kumshitaki Messi na baba yake kwa kushindwa kuweka wazi pato walilokuwa wakilipata haki za matangazo kati ya mwaka 2007 na 2009.

Kwa mujibu wa hati ya mashtaka, Messi na baba yake walikuwa na deni la kodi kiasi cha Euro 4.1 milioni ambazo sasa zilitakiwa kulipwa na nyongeza ya riba kwenye mahakama ili kuepukana na adhabu nyingine.

Hata hivyo kiujumla tatizo hilo halikuwaepusha na suala zima la kupelekwa mahakamani, na walifika mahakamani Juni 2, 2016 ikiwa ni siku chache kabla ya kuanza kwa mashindano ya Centennial Copa America ambako Messi alikuwa akijiandaa kwenda kuiwakilisha Argentina.

Messi aliweka wazi msimamo wake mbele ya Jaji pale aliposema, “Baba yangu ndiye anayehusika na masuala ya fedha, mimi nacheza soka.

Katika taarifa yake ya dakika 15 Messi alirudia kusisitiza mara kwa mara kwa kusema, “Namwamini baba yangu na wanasheria tuliowaajiri kulisimamia jambo hili, sijawahi na haijawahi kutokea wakaamua kuniweka pabaya”.

Messi pia alifafanua kwamba wakati wote alikuwa akienda kwenye ofisi ya wanasheria kusaini makubaliano bila kujua kilichomo ndani ya makubaliano hayo.

Alijieleza kwa namna ilivyotosha na baba yake alikuwa akimsaidia kwa kumpa baadhi ya mambo machache ya kuyasema.

“Nilijua kwamba tulikuwa tukisaini mikataba na wadhamini ambao wlaikuwa wakitoa kiwango X cha fedha na mimi nilikuwa na kazi ya kutoka hadharani, kupigwa picha na mambo kama hayo lakini sikuwa najua fedha zinakwenda wapi

Itaendelea Jumamosi ijayo…