Messi azua hofu Barcelona ikivaa Valencia

Muktasari:

Barcelona imekuwa ikiteseka sana kwa kucheza bila ya huduma ya Messi, ambapo wameshinda mara moja tu katika mechi nane alizokosa, ukijumlisha na zile za Novemba mwaka jana.

Barcelona, Hispania. Lionel Messi amewekwa kando kwenye kikosi cha Barcelona kitakachochuana na Valencia wikiendi hii, huku kukiwa na wasiwasi mkubwa kama Muargentina huyo atakuwa fiti kukipiga kwenye mechi ya kwanza ya Ligi ya Mabingwa Ulaya kutokana na kuwa majeruhi.

Messi, 32, bado hajaichezea mechi yoyote Barcelona msimu huu na ataendelea kuwa benchi kutokana na maumivu ya misuli ya kigimbi aliyopata kwenye kipindi cha mapumziko ya majira ya kiangazi.

Barcelona imekuwa ikiteseka sana kwa kucheza bila ya huduma ya Messi, ambapo wameshinda mara moja tu katika mechi nane alizokosa, ukijumlisha na zile za Novemba mwaka jana.

Kwa msimu huu, Barca wamekusanya pointi nne tu katika mechi zao tatu walizocheza kwenye La Liga bila ya huduma ya staa huyo. Kocha wa miamba hiyo ya Nou Camp, Ernesto Valverde alisema kwamba mshindi huyo mara tano wa Balon d'Or alipaswa kuwa fiti baada ya mapumziko ya mechi za kirafiki.

Lakini, kwa mazoezi ya Jumanne na Jumatano, Messi alionenkana akifanya kivyake kwa sababu bado hajapona vizuri. Kutokana na hilo, Messi hatarajiwi kuonenkana uwanjani kesho Jumamosi kwenye mchezo dhidi ya Valencia. Taarifa zaidi zinadai kwamba kocha Valverde hataki pia kumhatarisha Messi afya yake kwa kumpanga kwenye mechi ya kwanza ya Ligi ya Mabingwa Ulaya dhidi ya Borussia Dortmund.

Taarifa za karibuni zimedai kwamba kwenye mkataba wa Messi kuna kipengele kinachomruhusu kuondoka bure mwishoni mwa msimu. Mkataba wa sasa wa staa huyo utakomea 2021, huku Barca wakidaiwa kuwa na mpango wa kumpa Messi mkataba wa maisha.