Masoud alamba dili jipya

Muktasari:

Pia atapata fursa ya kushiriki dimba la CAF Champions League kutokana na Kabylie kuwa mabingwa watetezi wa Ligi Kuu ya nchini humo.

BAADA ya zaidi ya miezi saba bila klabu, straika wa Harambee Stars, Masoud Juma hatimaye kaangukia bahati na kusajiliwa na klabu moja ya kule Algeria Jeunesse Sportibe de Kabylie.
Kibarua cha Masoud cha mwisho kilikuwa na klabu ya Miliki za Kiarabu Dibba Fujairah kabla yake kuhamia Libya na kujiunga na Al Nasr.
Hata hivyo, kutokana na hali ya kivita nchini humo ligi  ya taifa hilo ilikosa kuanza na kusababisha kukatiza mkataba wake na Al Nasr. Sasa baada ya kukaa nje bila klabu kwa miezi saba Juma aliyejumulishwa kwenye kikosi cha Harambee Stars kilichokuwa Afcon licha ya kukosa soka la ushindani sasa atatimukia zake Algeria.
Klabu hiyo ilitangaza Jumapili imemsajili Juma kwa mkataba wa miaka mitatu na atakuwa m mmoja wa wachezaji wake tisa wapya iliyowasajili msimu  huu.
Pia atapata fursa ya kushiriki dimba la CAF Champions League kutokana na Kabylie kuwa mabingwa watetezi wa Ligi Kuu ya nchini humo.
Masoud aliikacha ligi ya Kenya 2017 baada ya kumaliza kama mfungaji bora kwenye msimu wake wa kwanza kwa kupachika magoli 17 akiichezea Kariibanghi Sharks.