Mashindano ya majiji kikapu kutimua vumbi Dodoma

Muktasari:

  • Mashindano hayo  ya kikapu yatafanyika Dododma na kushirikisha timu 14 za wanaume na wanawake kutoka katika majiji saba.

Dar es Salaam. Rais wa Shirikisho la mpira wa kikapu Tanzania (TBF) Phares Magesa ametangaza mashindano ya majiji Tanzania yatakayoanza Mei 8 mpaka 12, jijini Dodoma.

Magesa alisema mashindano hayo yatashirikisha timu 14 za wanaume na wanawake kutoka katika majiji ya Dar es Salaam, Mwanza, Arusha, Tanga, Mbeya, Zanzibar na Dodoma.

Katika hatua nyingine Shirikisho la Mpira wa kikapu FIBA Afrika, limemteua Prisca Boniface kuwa mmoja wa walimu watakaopata mafunzo jijini Windhoek Namibia, yatakayoanza Aprili 11 mpaka 13.

Kwa mujibu wa Rais TBF, Magesa alisema mafunzo hayo yatakuwa maalumu kwa watoto kuanzia miaka 3, lengo ni kuiendeleza vipaji vyao Tanzania na Afrika kwa ujumla.

"Tanzania tutawakilishwa na kocha Prisca haya ni mafunzo kwa makocha wote wa Afrika kila nchi inatoa kocha mmoja, fursa hiyo itatusaidia kuendeleza vipaji vya watoto nchini," alisema Magesa.