Mama wa bondia aliyemchakaza mzungu afunguka

Muktasari:

  • Amesema, mzee huyo ambaye kwa sasa ni marehemu, alikuwa anaupenda mchezo huo na wakati anarejea nchini akitokea Kuwait ambako aliishi kwa takribani miaka 10, alikuja na vifaa hivyo.

Tanga.  Mama mzazi wa Hassan Mwakinyo anayeitwa,   Fatma Hassan amefunguka mambo mazito kuhusu familia ya bondia huyo baada ya kumchakaza mzungu, Sam Eggington mjini Birmingham, England.

Fatma amesema, mchezo huo wa masumbwi upo katika damu ya familia na baba yake mzazi wa Mwakinyo ndiye aliyewaletea nyenzo kutoka nchini Kuwait.

Amesema, mzee huyo ambaye kwa sasa ni marehemu, alikuwa anaupenda mchezo huo na wakati anarejea nchini akitokea Kuwait ambako aliishi kwa takribani miaka 10, alikuja na vifaa hivyo.

“Alipofika tu na vifaa hivyo, alimkabidhi Hassan pamoja na kaka yake aitwaye Hamis Mwakinyo na vilikuwa kama urithi ambao matokeo yake ndiyo haya,”alisema Fatma akiwa maeneo ya nyumbani kwao Makorora Jijini Tanga.

Mama huyo alifafanua zaidi na kusema, wakati Mwakivyo anaondoka alimwomba mzazi wake huyo kumwombe kila siku.

"Nilizipokea taarifa hizo kwa furaha kubwa, yaani mtoto wangu ameshinda tena Uingereza ilikuwa ni kitu kipya na majibu mazuri ya dua zangu kwani nilikuwa nikiomba kila siku kama alivyoniomba,"alifafanua.

Hamis Mwakinyo ambaye ni kaka yake, Hassan Mwakinyo na pia ni kocha wa bondia huyo alisema, juhudi na nidhamu ya mazoezi ndiyo siri ya ushindi wake.