Majeruhi yamtibulia Msuva

WINGA James Msuva ambaye ni mdogo wa mshambuliaji wa Difaa El Jadida ya Morocco, ameamua kujiweka pembeni kwa muda kucheza soka kutokana na kuandamwa na majeraha ya nyama za paja.

James aliyekuwa KMC, tangu msimu huu uanze hajaonekana uwanjani na kikosi hicho na Mwanaspoti lilimtafuta kujua kulikoni wakati mwishoni mwa msimu uliopita alikuwa mmoja wa wachezaji waliokuwa wakipata nafasi kwenye kikosi cha kwanza cha timu hiyo ya Kinondoni.

Winga huyo alisema msimu huu amekaa pembeni kwanza mpaka katika dirisha dogo lijalo ndipo atajua nini ambacho anaweza kufanya, lakini muda huu ametenga kwa ajili ya kujitibia.

“Najitibia kwanza, ndio maana nimeona nitulie, mkataba wangu na wao tumevunja na ulikuwa umebaki mwaka mmoja, ila nitarudi nikiwa imara hapo baadaye,” alisema kwa kifupi.

Juu ya hofu ya kukosa nafasi kwenye timu 18 zinazoshiriki Lgi Kuu msimu huu, James aliyewahi kuchukuliwa na kaka yake nchini Morocco ili kutibiwa alisema: “Licha ya timu kupunguzwa bado inawezekana kurudi katika Ligi Kuu, timu 18 ni nyingi sana.”