Majeruhi ya Kane yazua hofu

Muktasari:

  • Kane alitarajiwa kuwa nje ya uwanja kwa miezi miwili, lakini sasa anatazamiwa kurudi uwanjani hivi karibuni kwa mujibu wa taarifa zilizofichuliwa na klabu yake ya Tottenham.

LONDON, ENGLAND.STAA wa Tottenham Hotspur, Gary Lineker amebainisha wasiwasi wake kuhusu majeruhi mfululizo ya enka yanayomkabili straika, Harry Kane.

Straika huyo Mwingereza, Kane anatarajia kurudi uwanjani baadaye mwezi huu baada ya kupata majeraha katika mechi dhidi ya Manchester United mwezi uliopita.

Lakini, Lineker amemtaka Kane kuyachukulia kwa umakini majeraha ya enka yanayomkabili mara kwa mara.

Lineker alisema: “Nimekuwa na wasiwasi kuhusu haya majeraha ya mara kwa mara ya enka. Inaonekana kuna tatizo mahali. Hakuna mchezaji anayetaka kuumia, lakini hapa inaonekana kuna udhaifu mahali.”

Kane alitarajiwa kuwa nje ya uwanja kwa miezi miwili, lakini sasa anatazamiwa kurudi uwanjani hivi karibuni kwa mujibu wa taarifa zilizofichuliwa na klabu yake ya Tottenham.

Kocha Mauricio Pochettino, anaamini straika wake anaweza kurudi uwanjani kuwakabili Burnley, Februari 23.

Tangu aanze soka la timu ya wakubwa, Kane amekumbana na majeraha ya enka mara nne tofauti jambo lililomfanya akose mechi 21.