MNGUTO: Yeye na karia mambo safi aahidi udhamini ligi zote- 2

Muktasari:

  • Amekiri kumwekea pingamizi Kimbe kwa maelezo Kimbe alikuwa ni Mkurugenzi na Mwenyekiti wa Mbeya City.

“HII nafasi nimeitafuta kwa utashi wangu mwenyewe, Karia kaniunga mkono kwasababu tunafahamiana na mipango yangu na yake inaenda sawa, nafurahi kufanyakazi na mtu ninayemfahamu nitakuwa na nafasi kubwa ya kumshauri mazuri na kumkataza asifanye vitu ambavyo havina maendeleo katika soka,”.

PINGAMIZI YA KIMBE

Amekiri kumwekea pingamizi Kimbe kwa maelezo Kimbe alikuwa ni Mkurugenzi na Mwenyekiti wa Mbeya City.

“Kwa mujibu wa sifa zinazotakiwa kwa mjumbe anayetakiwa kuiongoza Bodi ya Ligi ni yule ambaye ni mwenyekiti wa klabu lakini yeye alikuwa na nafasi mbili kitu ambacho ndio kilinifanya nimuwekee pingamizi na kama saizi ni mwenyekiti tu, basi amefanya mabadiliko sasa,” alisema.

FDL, SDL KUKOSA UDHAMINI

Ligi hizo mbili hazina mvuto, uchezeshwaji mbovu wa ligi yenyewe, hazina utaratibu unaoeleweka wa kiuendeshaji kwa maana hiyo hawajajipanga kwaajili ya kuhakikisha timu zinapata matokeo mazuri.

Kutokana na changamoto hiyo anasema chini ya utawala wake atahakikisha anapambana kuondoa changamoto hiyo na kuweka wazi kuwa tayari Karia yupo katika hatua nzuri za mazungumzo na moja ya kampuni ambayo itawekeza Ligi Luu, Ligi Daraja la Kwanza na la Pili.

WAPI TFF WANAKOSEA KUPATA UDHAMINI

Anafafanua hawezi kusema wanakosea wapi kwasababu sababu zipo wazi ambazo ni pamoja na makampuni kushindwa kuendana na thamani ya ligi yenyewe.

“Hatutakiwi kutoa lawama tunatakiwa kuangalia hali ya kiuchumi ilivyoyumba ambayo kwa kiasi kikubwa ndio imechangia kukosekana kwa mdhamini mfano tulikuwa na Vodacom wameshindwa kuongeza kiasi cha fedha walichokuwa wanatoa misimu iliyopita na kuomba kupunguza kitu ambacho hakiwezekani kwa ongezeko la timu,” alisema.

KAMPUNI KUWEKEZA

“Kufuata mfumo kama Kenya hatufikirii na wala hatuwezi kufanya hivyo kwasababu huko tu kulitokea mgawanyiko wakawa na ligi mbili hatutaki kufika huko malengo yetu ni kuwa na ligi ya ushindani.

“Tanzania inaongozwa na TFF, hivyo tunatakiwa kufanya kazi sambamba na shirikisho, Mwenyekiti wa Bodi ya Ligi lakini nashauriwa na Karia nikitaka kwenda kinyume na huyo, basi natengeneza matabaka,” alisema Mguto.

ALIDHAMILIA TPLB

“Hakuna changamoto yoyote kwa mimi kuchaguliwa kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Ligi kwasababu nilidhamiria kuwania na kuwa kiongozi.

“Nakumbuka nilianza kuipenda Coastal Union tangu mwaka 1965 lakini sikuwahi kugombea uongozi katika klabu hiyo, kuna kipindi upepo ulikuwa mbaya kwao timu ikawa inafanya vibaya kutokana na mapenzi yangu, nilifuatilia sababu na kubaini kuwa tatizo ni uongozi.

“Mwaka 2009 niliamua kugombea uongozi na nilichaguliwa, nilipoingia madarakani nilipambana kuhakikisha naipandisha timu Ligi Kuu kitu kilichonifanya nifanye hivyo ni dhamira,”.

Amesema hata Bodi ya Ligi ni dhamira iliyomsukuma afanye hivyo na kuweka wazi kuwa sio kwamba anaona mambo yanaenda vibaya katika bodi, bali anataka kusaidiana nao ili kufikia mafanikio.

“Kabla sijachaguliwa miaka mitano iliyopita nilihusika kuunda Bodi ya Ligi naifahamu vizuri waliopita walifanya mazuri pia kuna makosa wamefanya japo ni ya kuyachukulia kama shule sio ya kunyosheana vidole,” alisema.

Anasema anaamini bado ana mchango mkubwa wa kuendeleza mazuri aliyoyakuta na kuongeza mengine bora zaidi ili kuweka mchango wake katika bodi hiyo.