M-Bet yawazadia mashabiki wa Real Madrid, Barcelona

Ushindi wa mabao 3-1 wa Real Madrid dhidi ya mahasimu wao, Barcelona ulinongeshwa na chemsha bongo ya kampuni ya michezo ya kubahatisha ya M-Bet Tanzania na mashabiki wa soka kujishindia zawadi mbalimbali.

Tukio hilo lilifanyika kwenye baa ya Tips ya Mikocheni ambapo mbalimbali ya mashabiki kuzawadiwa zawadi mbalimbali zikiwemo jezi orijino za timu hizo mbili, pia waliweza kupiga picha na kombe ‘replica’ la La Liga ambalo Real Madrid ilishinda msimu uliopita.

Mabao ya Real Madrid yalifungwa na  Federico Valverde, Sergio Ramos (kwa njia ya penati) na Luka Modric wakati lile la kufutia machozi la Barcelona lilifungwa na Ansu Fati.

Meneja Masoko wa kampuni ya M-Bet Tanzania, Allen Mushi alisema kuwa wameamua kuwachangamsha mashabiki wa soka ligi ya Hispania kutokana na ushirikiano wao na La Liga.

Mushi alisema kuwa  wameamua kuwazawadia mashabiki wa soka kama kutambua mchango wao katika shughuli zao za michezo ya kubahatisha.

Alisema kuwa maswali yao mengi yamelenga ufahamu kuhusiana na La Liga kama mchezaji gani aliyefunga mabao mengi, wachezaji maarufu waliocheza ligi hiyo, mchango wa Cristiano Ronaldo na Lionel Messi katika timu zao, umaarufu wao na makocha.

“M-Bet imeingia mkataba na La Liga katika kuendeleza soka la vijana ili kuleta maendeleo ya soka kwa timu zetu na timu ya Taifa, kabla ya kuanza kuendesha mafunzo mbalimbali, tumeamua kuanza kutoa zawadi kwa mashabiki

Mbali ya mechi ya El Clasico, tutaendelea kutoa zawadi katika mechi nyingine mbalimbali za ligi ya Hispania na kutoa eleimu ya ufahamu wa ligi hiyo kwa mashabiki wa soka,” alisema.