Lwandamina: Sitaki kuahidi maajabu kwa Mazembe

Muktasari:

Mshindi wa mechi kati ya Zesco United na TP Mazembe atakata tiketi ya moja kwa moja kucheza hatua ya makundi ya Ligi ya Mabingwa, wakati yule atakayefungwa ataingia katika hatua ya mtoano Kombe la Shirikisho Afrika

Lusaka, Zambia. Kocha wa zamani wa Yanga, George Lwandamina amesema hawezi kuhaidi timu yake Zesco United kwamba itashinda mchezo wao wa ugenini dhidi ya TP Mazembe katika Ligi ya Mabingwa.

Mabingwa hao wa Zambia, Zesco United imefanikiwa kusonga mbele katika mashindano hayo baada ya kuwatoa mabingwa wa Niger, AS Sonidep kwa jumla ya mabao 5-1 na kupata tiketi ya kuwavaa miamba hiyo DR Congo, TP Mazembe.

Kocha Lwandamina akizungumza baada ya mechi yake iliyofanyika kwenye Uwanja wa Levy Mwanawasa, Ndola alisema hawezi kuhaidi miujiza ukizingatia kuwa tutacheza dhidi ya TP Mazembe lakini ndiyo njia yenyewe, siwezi kuruka kihunzi hiki.

Lwandamina alisitiza bado hajafikia katika malengo yake anayotaka. Alisema baada ya ushindi katika mchezo wa kwanza nchini Niger mechi ya marudiano ilikuwa ni bonasi.

“Kuhusu TP, tutacheza nao ugenini. Kwa sababu siwezi kuruka bunduki. Tutafanya mambo yetu kwa mahesabu, hadi pale tutakapofikia tunapotaka. Ila sitaki kuwahaidi watu kuwa tutafanya maajabu, kutoke wapi?,” alisema Lwandamana.

“Kisayansi hakuna linaloshindika, lakini hapa kuna watu wanaofanya kazi. Kwahiyo tutaenda kimahesabu, hadi tutakapofikia mwisho. Kama tutashinda mechi yetu ya ugenini basi hiyo itakuwa ni kazi ya wachezaji.”

“Timu bado tupo katika kipindi cha maandalizi ya msimu mpya. Kwa hiyo ushindi utakuwa ni bonsai kwa wachezaji katika kipindi hiki cha maandalizi ya msimu mpya.”