Leyla amekubali kila kitu kwa Mzee Yusuf

Muktasari:

MWIMBAJI mahiri wa muziki wa taarabu na mke wa Mzee Yusuf, Leyla Rashid ameeleza namna wamepitia kipindi kigumu baada ya mume wake kutangaza kurudi kwenye muziki.

MWIMBAJI mahiri wa muziki wa taarabu na mke wa Mzee Yusuf, Leyla Rashid ameeleza namna wamepitia kipindi kigumu baada ya mume wake kutangaza kurudi kwenye muziki.

Leyla ameyasema hayo kwenye mahojiano na Mwanaspoti, wakati wa shoo ya Mzee Yusuf ya 'Narudi Mjini' iliyofanyika jijini Dar es Salaam baada ya kuacha kazi hiyo miaka minne iliyopita.

Onyesho hilo ambalo Mzee Yusuf ni la kwanza kulifanya tangu alivyotangaza kurudi kwenye muziki, Machi mwaka huu, lililenga kukutana na mashabiki zake kuwasalimia.

Akizungumza namna walivyopokelewa tangu mumewe alipotangaza kurudi kwenye muziki, Leyla amesema amekuwa akiyaoga matusi hususani mitandaoni kwa kila wanachoweka jambo ambalo anashukuru ameweza kulihimili japokuwa mengine huwa akilazimika kuwajibu watu.

"Kweli kama ni matusi nimeyapata sana kutokana na maamuzi ya Mme wangu kurudi kwenye muziki, na yanaumiza haswa lakini sina budi kukubaliana nayo, kwa kuwa hakuna anayejua tunapitia nini zaidi ya Mwenyezi Mungu, hivyo acha wanadamu waendelee kutuhukumu kwa kuwa tunafanya kwa ajili ya familia yetu," amesema Leyla.

Hata hivyo hakusita kuonyesha furaha yake ya namna walivyopokelewa na kusema kimewafanya kujua kuwa Mzee Yusufu bado anakubalika katika muziki huo.

Katika onesho hilo lililoanza saa 4:00 na kumalizika saa tisa usiku, Leyla alimsindikiza mume wake huyo kwa kuwakonga nyoyo mashabiki hasa pale walipowakumbushia nyimbo za zamani ikiwemo 'sina muda huo', Mpenzi Chocolate na VIP.

Pia waliimba kwa mara ya kwanza nyimbo yao mpya waliyoiimba kwa kushirikiana na Mzee Yusuf inayoitwa Full Dose na vibao vingine walivyoviachia ndani ya wiki hii ikiwemo Najilipua, Ndio Yaleyale na Wanakereketwa.