Lacazette naye karudi, Rennes mbona sasa watateseka

Muktasari:

  • Kurejea kwa Lacazette kunampa nguvu kubwa Kocha Unai Emery na kuamini fowadi yake itakuwa kwenye makali ya kuhakikisha Wafaransa wanateseka na kushinda kwenye mechi hiyo ya maruduano.

LONDON, ENGLAND. ARSENAL inachekelea baada ya kuruhusiwa kumtumia straika wake matata kabisa, Alexandre Lacazette kwenye mchezo wa leo Alhamisi dhidi ya Rennes huko kwenye Europa League.

Straika huyo awali alifungiwa mechi tatu baada ya kuonyeshwa kadi nyekundu katika mechi ya hatua ya 32 bora dhidi ya BATE Borisov, lakini sasa Uefa imepunguza adhabu hiyo na kuwa mechi mbili, ambazo kimsingi ameshazitumikia, hivyo atakuwa huru kukipiga kwenye mechi ya maruduano itakayopigwa uwanjani Emirates.

Kwa adhabu ya awali, Lacazette asingecheza mechi hiyo ya huko Emirates dhidi ya Rennes, ambapo Arsenal itaingia uwanjani ikiwa na kazi moja tu ya kufanya kupindua matokeo baada ya kuchapwa 3-1 huko Ufaransa.

Kurejea kwa Lacazette kunampa nguvu kubwa Kocha Unai Emery na kuamini fowadi yake itakuwa kwenye makali ya kuhakikisha Wafaransa wanateseka na kushinda kwenye mechi hiyo ya maruduano.

Lacazette amekuwa chaguo la Emery kwenye fowadi ya timu hiyo kwa siku za karibuni akipewa nafasi kubwa ya kucheza mbele ya straika Pierre-Emerick Aubameyang.