Kwa staili ya Cioba ,Azam FC itafanya maajabu makubwa

Muktasari:

Kwa mtazamo wangu, suala la Azam kufanya vizuri kwa sasa limekuwa ni mtambuka kwa sababu mabadiliko ya kocha wameyafanya katika kipindi ambacho baadhi ya klabu pia zimefanya kitu kama hicho. Ndio, Yanga na klabu zingine wamefanya mabadiliko kama hayo.

TUNAELEKEA katika mashindano ya Kombe la Chalenji ambayo yanashirikisha nchi wanachama wa Baraza la Vyama vya Mpira wa Miguu Afrika Mashariki na Kati (Cecafa).

Mashindano hayo yamepangwa kuanza Disemba 7 na yatafikia tamati mnamo Disemba 19 mwaka huu na yatafanyika nchini Uganda yakishirikisha jumla ya nchi 12 zinazounda baraza hilo. Nchi hizo ni Uganda, Burundi, Ethiopia, Eritrea, DR Congo, Sudan, Sudan Kusini, Somalia, Kenya, Djibout, Tanzania Bara na Zanzibar.

Kutokana na uwepo wa mashindano hayo, Ligi Kuu Tanzania Bara ambayo imefikia katika raundi ya 13 hivi sasa, itasimama kwa muda ili kuipa nafasi timu ya taifa ya Tanzania Bara ‘Kilimanjaro Stars’

Zipo timu ambazo licha ya kutoanza ligi vizuri msimu huu katika siku za hivi karibuni zimekuwa moto wa kuotea mbali na miongoni mwa hizo ni Azam FC. Hawa jamaa ni wazuri sana. Timu hiyo imepata ushindi katika michezo mitatu mfululizo iliyopita dhidi ya Biashara United, Mbao FC na Alliance FC.

Lakini, sio ushindi tu bali pia imekuwa ikionyesha kiwango kizuri ambacho kimekuwa gumzo kwa mashabiki wa soka nchini na imekuwa ikitengeneza idadi kubwa ya nafasi za mabao tofauti na ilivyokuwa siku za nyuma.

Hapana shaka hilo kwa kiasi kikubwa limechangiwa na kocha Aristica Cioaba, ambaye alijiunga na timu hiyo miezi kadhaa iliyopita, akichukua nafasi ya Etienne Ndayiragije ambaye kwa sasa amepewa jukumu la kuinoa timu ya taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’.

Wengi wanaweza kujiuliza siri ya kufanya vizuri kwa Azam katika siku za hivi karibuni huku ikiwa na kocha, ambaye hajapata muda wa kutosha kuijenga timu tangu alivyopewa nafasi huku ligi ikiwa inaendelea.

Kwa mtazamo wangu, suala la Azam kufanya vizuri kwa sasa limekuwa ni mtambuka kwa sababu mabadiliko ya kocha wameyafanya katika kipindi ambacho baadhi ya klabu pia zimefanya kitu kama hicho. Ndio, Yanga na klabu zingine wamefanya mabadiliko kama hayo.

Kwa kiasi kikubwa suala la molali ndilo linaweza kuwa chanzo cha Azam FC kuwa moto wa kuotea mbali. Hizi timu zinapofanya vibaya, kuna matatizo ambayo sisi wa nje tunayaona lakini pia kuna mengi tusiyoyajua lakini waliomo ndani wanayafahamu.

Sasa Cioaba aliwahi kufundisha Azam na anaifahamu vyema kuanzia wachezaji, utamaduni hadi ‘management’ yake hivyo pengine imekuwa rahisi kwake kufahamu tatizo na kulifanyia kazi jambo ambalo pengine limesaidia kuamsha morali ya timu.

Kuna wachezaji ambao walikuwa hwatumiki vizuri wakati wa nyuma lakini Cioaba amejua anawatumia vipi ili kumpa matokeo mfano mshambuliaji Obrey Chirwa hii tunaita ‘coaching philosophy’ au coaching professionalism’.

Lakini, kingine ambacho nakiona ni kuwatumia vizuri wachezaji jambo ambalo limepelekea hata wale ambao, waliokuwa hawapati nafasi awamu iliyopita waanze kupata sasa. Kwa falsafa kama hiyo wachezaji hujenga morali ya kupambana na hapo unapata matokeo mazuri ndani ya uwanja.

Pamoja na hilo, mbinu zake nazo zinaweza kuwa chachu ya Azam kufanya vizuri. Cioaba ni mwalimu ambaye muda wote amekuwa akifundisha soka la kucheza kwa nafasi, lakini pia matumizi ya hizo nafasi kupata mabao. Kwa hiyo kikubwa ni kwamba morali imewafanya wachezaji wa Azam kubadilika na kadri wanavyocheza, wanazidi kupata muunganiko mzuri ambao unakuwa chachu kwao kufanya vizuri.

Lakini, kuna timu tatu ambazo ni Singida United, Mbeya City na Ndanda FC. Hizi zimekuwa hazifanyi vizuri na ninachokiona, sababu inayopelekea hilo ni mabadiliko ya mara kwa mara ya makocha ambayo timu zetu zimekuwa zikifanya. Makocha waliopo wamezikuta hizo timu na hawajakaa kwa muda mrefu na walikabidhiwa jukumu hilo baada ya makocha waliowatangulia kutimuliwa.

Matokeo yake timu hizo zimekosa ‘stability’ kwa sababu zipo katika ‘transition’ na kujikuta hazifanyi vizuri. Tusubiri katika dirisha dogo kuona zitafanya nini pengine zinaweza kufanya usajili wa maana wa kuziimarisha lakini hilo litategemea hali zao za kiuchumi. Lakini, kama zisipokuwa na mabadiliko ya kiutendaji, hizo timu zitashuka kwa sababu kadri ambavyo zinafungwa, zinasababisha ‘confusion’.

Kikubwa zinapaswa kipindi cha dirisha dogo na mapumziko ya ligi kufanya ‘post analysis’ au post evaluation’ ili kuona zitafanya nini katika usajili.