Kwa Yanga hii mtapata tabu sana!

Muktasari:

KOCHA Mkuu wa Yanga, Zlatko Krmpotic amewashusha presha mashabiki wa timu yake akiwaambia mabao yatakuja, kwani kilichomuhimu kwake kwanza ni kuvuna alama tatu muhimu ili kujiweka pazuri na kusema wapinzani wao watapata tabu sana juu yao.

KOCHA Mkuu wa Yanga, Zlatko Krmpotic amewashusha presha mashabiki wa timu yake akiwaambia mabao yatakuja, kwani kilichomuhimu kwake kwanza ni kuvuna alama tatu muhimu ili kujiweka pazuri na kusema wapinzani wao watapata tabu sana juu yao.

Yanga katika mechi zao tatu za awali za Ligi Kuu Bara mpaka sasa imefunga mabao matatu, huku nikiruhusu moja na kutowapa furaha mashabiki wao kutokana na majembe iliyonayo kikosini, lakini Kocha Zlatko amewatuliza akiwaaambia anaijenga kwanza timu.

Akizungumza jana mara baada ya kurejea jijini Dar es Salaam wakitokea Bukoba walipowachapa Kagera Sugar kwa bao 1-0, kocha huyo alisema hata yeye hakubaliani na kasi ndogo ya ufungaji mabao kwa ubora wa kikosi chake, lakini anajua mambo yanajengwa taratibu na Yanga itatisha.

Kocha Zlatko alisema bado anataka kuona kikosi chake kinatumia zaidi nafasi wanazotengeneza uwanjani, lakini timu inaposhinda ni hatua muhimu kwa kuwa sio rahisi kupata matokeo.

“Siwezi kuridhika na kila kitu, lakini nafurahi kuona timu inashinda kwa sasa tukiwa nyumbani na hata ugenini. Sio rahisi lakini narudia hapa bado tunatengeneza timu mambo mazuri hayawezi kuja kwa haraka sana,” alisema Zlatko ambaye timu yake imeshinda mbili na kutoa sare moja.

“Kuna wakati tunatakiwa tutumie zaidi nafasi tunazotengeneza katika mechi, angalia jana (juzi) kuna nafasi ya uhakika Carlinhos (Carlos Fernandez) aliipoteza hili sio zuri, lakini bado kuna kazi tunatakiwa kuifanya na wapinzani wetu wajiandae kupata tabu ikiimarika zaidi.

Aidha kocha huyo kwa sasa wanaingia katika maandalizi ya mchezo unaofuatia dhidi ya Mtibwa Sugar, akidai Ligi Kuu Bara, hakuna mechi rahisi kutokana na wapinzani wao nao wanajiandaa vyema kuhakikisha wanawazuia lakini anafurahi kuona morali ya nyota wake ipo juu.

“Nafurahia kuona wachezaji wangu sio watu wanaokata tamaa,nidhamu yao ya kupambana ipo juu sana narudia kusema hii ni timu mpya kuna mambo yatakuwa sawa taratibu hatujacheza mechi rahisi mpaka sasa kila mechi ina ugumu wake.”

MWAMNYETO AKIPIGA KIJEMBE

Katika hatua nyingine beki wa kati wa Yanga, Bakar Mwanyeto amesema amesikia kelele za mashabiki wa Simba alishika mpira na mwamuzi kuwanyima penalti Kagera, kisha kuwaambia Wekundu wa Msimbazi hao ‘hakuna kitu kama hicho, nyie pambaneni na hali zenu’.

Tukio la dakika ya 46 ya nyongeza kipindi cha kwanza krosi ya mshambuliaji Vitalis Mayanga ilionekana kama imemgonga Mwamnyeto katika mkono wake wa kulia na tukio hilo lilitafsiriwa ameushika na mwamuzi kukausha.

Hata hivyo, akizungumza jana, Mwamnyeto alisema ameona mijadala hiyo kupitia mitandao ya kijamii, ila sio kweli kama mpira ulimgonga katika mkono wake na wala hakukaribia.

“Mpira hakufika kabisa mkononi, nimeona hilo watu wanasema lakini ukweli ni kwamba mpira haukunifikia kabisa katika eneo la mkono hao wanaosema kazi kwao,” alisema Mwamnyeto.

Beki huyo ghali nchini alisema kwa wachezaji wazawa alisema alikuwa makini katika shambuliao na namna ile na alitangulia kuuficha mikono yake nyuma, ingawa baadaye aliachia baada ya kuona mpira haukaribii mikono yake.

“Watu watulie wanapoliangalia lile tukio unajua kwanza nilianza kuweka mikono nyuma, lakini nilipoona mpira hauwezi kunifikia mikononi nikaiachia na ukanigonga kifuani pembeni kidogo.”

Alisema kwa nafasi ambayo mwamuzi wa kati alikuwa amesimama isingekuwa tabu kwake kuliona tukio hilo na wala halimchanganyi na ana uhakika hakuunawa.