Kwa Tambwe ni moto tu unaambiwa!

Muktasari:

Amissi Tambwe ambaye ni Mrundi, amekuwa kwenye mahusiano na Raiyan kwa kipindi cha takribani miaka mitano na wamefanikiwa kuzaa mtoto mmoja wa kiume anayeitwa, Ayman.

 

Dar es Salaam. Sherehe na mpango mzima wa ndoa ya mshambuliaji wa Yanga, Mrundi Amissi Tambwe zimeendelea kufana ambapo jana Jumatano ilidamshi Singo ya kina mama iliyoongozwa na mkewe, Raiyan Mohammed  maarufu kwa jina la Ray wa Tambwe.

Wakati sherehe hizo zikiendelea kubamba harusi itakuwa leo Alhamisi pale maeneo ya Buguruni jijini Dar es Salaam.

Katika sherehe ya Singo inayowahusisha wanawake kama Kitchen Part ilifanyika maeneo ya Kariakoo na wanawake walitokelezea kwa wingi.

Wengi wao walikuwa ni wake wa wachezaji wa mpira kama mke wa nahodha na beki wa Yanga, Kelvin Yondani 'Vidic' anayeitwa Nance Mussa na wa Geofrey Taita wa Kagera Sugar, Ashama Mabrock.

Raiyan alikuwa amevaa gauni lenye rangi ya pinki lililopambwa na malembo mbalimbali na lilimpendeza pamoja na mapambo tofauti aliyopambwa.

Katika uso wake, alikuwa amevaa kitu mfano wa kitambaa chepesi chenye urembo kilichokuwa kimeficha baadhi ya sehemu ya uso wake.

Baada ya tukio hilo, kinachofata ni ndoa ambayo itakuwa ya Kiislamu na  inatarajiwa kufungwa leo maeneo ya Buguruni.