Kwa Kaseke nidhamu ndo mpango mzima unaambiwa

Muktasari:

Kaseke alisema kwake anaona kucheza na Leopards ama timu yoyote haiwezi kuwa na tija kama wachezaji wa timu hawana nidhamu, ikiwa kama nyota wa Msimbazi ambao walienguliwa kikosi cha Taifa Stars kwa kuchelewa kambini.

WINGA wa Yanga, Deus Kaseke amecheka sana baada ya kuzisikia kejeli ya mashabiki wa Simba wajisifu juu ya timu yao jana kuvaana na AFC Leopards ya Kenya na kuliponda chama lake ambalo leo JUmapili linavaana na African Lyon.

Kaseke alisema kwake anaona kucheza na Leopards ama timu yoyote haiwezi kuwa na tija kama wachezaji wa timu hawana nidhamu, ikiwa kama nyota wa Msimbazi ambao walienguliwa kikosi cha Taifa Stars kwa kuchelewa kambini.

Kauli ya Kaseke ilikuja baada ya kuulizwa anajisikiaje wapinzani wao Simba kujipima ubavu na AFC Leopards, huku wao wakicheza na African Lyon na kuanza kwa kicheko kisha akasema; “Yaani wewe una nongwa naona kawaida tu.”

“Timu yoyote inayocheza Ligi Kuu inatakiwa kuheshimiwa na ndio maana nimeeleza kuwa katika soka nidhamu ndio msingi wa soka yaani ni kila kitu, kama wachezaji hawana nidhamu wala kuheshimu wapinzani wao hawafiki mbali,” alisema Kaseke. Alisema Lyon ni timu ya Ligi Kuu sawa tu na Leopards wanaotokea Kenya, hivyo watavaana nao waliiheshimu kwa vile ndio utamaduni wa Yanga .

“Mfano mzuri tuliweka kambi Morogoro, wenzetu walienda Uturuki, majibu ya mechi za kwanza hatuchekani, tulishinda 2-1 dhidi ya Mtibwa Sugar, wao wakaifunga Prisons 1-0 kabla ya kuilaza Mbeya City 2-0, hivyo hatuchekani,” alisema bila kufafanua.

Naye straika wa timu hiyo, Emmanuel Martin alisema anayekosa ndiye anatafuta kwa bidii, akifafanua kuwa pamoja na picha inayotazamwa na wadau wa soka kuhusu Yanga hiyo ni sababu ya wao kujituma.

“Asikwambia mtu kuna tofauti ya juhudi ya utafutaji kwa mtu mwenye njaa na aliyeshiba.”