Kumekucha Simba, Yanga, Azam Kombe la Mapinduzi

Muktasari:

Timu 10 zikitarajiwa kushiriki ambapo timu 6 kutokea Zanzibar, 3 kutoka Tanzania Bara na 1 kutokea nchini Uganda.

Kamati ya kusimamia Mashindano ya Kombe la Mapinduzi (Mapinduzi Cup) ya mwaka 2019 imetangazwa rasmi leo na Katibu Mkuu wa Wizara ya Vijana Utamaduni Sanaa na Michezo Omar Hassan (King) ambayo itaongozwa na Mwenyekiti Sharifa Khamis (Bi Shery).
Akitangaza Kamati hiyo Katibu King amesema Mashindano hayo yanatarajiwa kuanza Desemba 30, 2018 na kumalizika Januari 13, 2018 kwenye uwanja wa Gombani Kisiwani Pemba huku timu 10 zikitarajiwa kushiriki ambapo timu 6 kutokea Zanzibar, 3 kutoka Tanzania Bara na 1 kutokea nchini Uganda.
Timu zitakazoshiriki ni Malindi, Mlandege, KMKM, KVZ (Unguja) nyengine ni Jamhuri na Chipukizi (Pemba) ambapo kutoka Tanzania bara ni Simba, Yanga na Azam huku URA kutokea Uganda nayo ikitarajiwa kushiriki kwenye Mashindano hayo.
Kamati hiyo itaongozwa na Mwenyekiti Sharifa Khamis (Bi Shery), Khamis Ali Mzee (Makamo Mwenyekiti) huku wajumbe wakiwa ni Iman Duwe, Mohammed Ali Hilali (Tedy), Mwalim Ali Mwalim, Khamis Abdallah Said, Ali Khalil Mirza, Ambar Sharif,  Issa Mlingoti, Mzee Ali Abdallah, Fatma Rajab Hamad, Abubakar Bakhresa na Juma Mmanga.