Kumbe janja ya Wawa ni hapa!

Muktasari:

  • Simba itacheza mechi yake ya pili hatua ya makundi ya Ligi ya Mabingwa Afrika Januari 19, nchini Congo dhidi ya Vita Club. Simba ndiyo  vinara wa Kundi D, wakiwa na pointi tatu sawa na Al Ahly ya Misri iliyo ya pili wakitofautiana idadi ya mabao, Vita Club ya tatu haina pointi sawa na JS Saoula ya Algeria iliyo nafasi ya nne.

Dar es Salaam. Ebwana wale ambao wanataka kumfahamu vizuri beki wa Simba, Muivory Coast Pascal Wawa unaambiwa hivi ni katika mechi za kimataifa.

Wawa ambaye kikosi chake kinacheza mechi za makundi ya Ligi ya Mabingwa Afrika ikiwa kimepangwa Kundi D, pamoja na timu za AS Vita ya Congo, Al Ahly ya Misri na JS Saoula ya Algeria.

Beki huyo ambaye awali alikuwa akicheza pacha na Erasto Nyoni na sasa Juuko Murshid raia wa Uganda, wakati mwingine anapocheza mechi za ndani za Ligi Kuu anakuwa kama hayuko sawa lakini utofauti wake huwa unaonekana katika michezo ya kimataifa ambayo huwa anang'ara.

Kitendo hicho kimemfanya beki wa zamani wa Yanga, Bakari Malima 'Jembe Ulaya' atamke neno: "Ukitaka kumpenda na kufurahia kiwango cha Wawa ni kwenye mechi za kimataifa hapo ndiyo mahala pake."

Amesema, kipimo hicho ndiyo kinachomtofautisha na mabeki wengine kutokana na namna anavyojituma, kucheza kwa akili na nguvu.

Simba inaendelea na michuano hiyo ambayo wameanza vizuri na kushinda mchezo wao wa kwanza dhidi ya JS Saoula kwa kuichapa jumla mabao 3-0, Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.