Kocha wa Alliance FC aihofia Yanga mapema

Muktasari:

Alliance wataingia katika mchezo huo wakiwa na kumbukumbu ya kufungwa mabao 5-0 na Azam FC kwenye Uwanja wa Nyamagana

Mwanza. Kocha wa Alliance FC, Kessy Mziray amesema Yanga ni timu kubwa hivyo wataingia kwa tahadhali katika mchezo wa kesho saa 10:00 jioni kwenye Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza.

Akizungumza leo, jioni, Mziray amesema maandalizi yao yamekamilika, kwahiyo hawatarajii kufanya makosa kama yaliyotokea katika mchezo uliopita dhidi ya Azam waliofungwa mabao 5-0.

"Yanga ni timu kubwa lazima tuwape heshima yao, lakini na sisi tumejipanga kuhakikisha tunaenda kuibuka na ushindi, maandalizi yamekamilika kuelekea katika pambano hilo" amesema Mziray.

Aidha Mziray amesema mbali na wachezaji wake ambao wapo kifunguoni wakitumikia adhabu ya  kadi nyekundu John Mwanda na Israel Patrick, wengine wote wapo fiti kucheza mechi hiyo muhimu kwa timu zote.

Alliance wataingia katika pambano hilo la kesho wakiwa na kumbukumbu mbaya ya kufungwa mabao 5-0 kutoka kwa Azam FC katika Uwanja wa Nyamagana huku Yanga wao wakikumbuka ushindi wa mabao 3-2 dhidi ya JKT Tanzania.