Kocha Harambee Stars afichua sababu za kumtema Were

Muktasari:

Kenya inamenyana na Ghana alasiri ya leo mjini Accra kwa mechi ya raundi ya mwisho kufuzu kombe la mataifa bora barani (AFCON) kwanzia saa tatu usiku.

KOCHA wa timu ya taifa ya Kenya, Harambee Stars, Sebastien Migne amefichua sababu za kumtema straika, Jesse Were kwenye kikosi cha wachezaji 22 kilichosafiri nchini Ghana.

Kenya inamenyana na Ghana alasiri ya leo mjini Accra kwa mechi ya raundi ya mwisho kufuzu kombe la mataifa bora barani (AFCON) kwanzia saa tatu usiku.

“Were ni mchezaji mzuri mwenye kujituma uwanjani lakini sijaona kama amefika levo yetu licha ya kufanya vyema Ligi ya Zambia lakini huwezi kulinganisha mechi za kimataifa za haiba kubwa na Ligi ya Zambia,” alisema.

Maoni hayo ya Migne yamepingwa vikali na wadau wa soka akiwemo straika wa zamani wa Harambee Stars, Boniface Ambani. “Kocha ana haki ya kuamua ni mchezaji yupi atatumia lakini rekodi za mchezaji huwa muhimu sana kwani timu ya taifa ni ya nyota wanaofanya kweli kwenye klabu zao na Were ameonyesha hili, ni makosa kumtema mchezaji kama huyu haswa wakati tegemeo Michael Olunga hayupo,” alisema Ambani kwa hamaki.

Migne alisafiri na washambulizi watatu; Allan Wanga ambaye ni mfungaji bora katika ligi ya Kenya msimu huu. Masoud Juma hajakuwa akicheza kwani alijiunga na kilabu ya Libya Al Nassr na Piston Mutamba wa Sofapaka.