Kilimanjaro Stars, Zanzibar Heroes kumalizana mapema Cecafa

Muktasari:

Kenya ndio bingwa mtetezi wa mashindano ya Cecafa Chalenji baada ya kutwaa taji hilo mwaka juzi kwa kuichapa Zanzibar kwa ushindi wa mikwaju ya penati 3-2 baada ya timu hizo kumaliza dakika 90 za mchezo wa fainali kwa sare ya mabao 2-2.

Dar es Salaam.Wakati mashindano ya Chalenji yanayosimamiwa na Baraza la Vyama vya Mpira wa Miguu Afrika Mashariki na Kati (Cecafa) yakitarajiwa kuanza Jumamosi nchini Uganda, timu za taifa za Tanzania Bara 'Kilimanjaro Stars' na Zanzibar 'Zanzibar Heroes' zimepangwa kukutana katika mchezo wa ufunguzi wa kundi C.

Mechi hiyo itachezwa Jumapili saa 10 jioni jijini Jinja mara baada ya kumalizika kwa mchezo wa kwanza wa kundi hilo baina ya Kenya na Djibout ambao utachezwa kuanzia saa 8.30 mchana.

Kutokana na uhusiano na kufahamiana vyema kwa wachezaji timu hizo mbili mbili zimekuwa na ushindani mkali pindi zikutanapo huku Zanzibar wakiwa na kumbukumu nzuri ya kuibuka na ushindi katika mchezo wa mwisho uliozikutanisha mwaka juzi wakishinda kwa mabao 2-1.

Kwa mujibu wa ratiba iliyotolewa na Cecafa leo, mechi ya ufunguzi itakuwa ni baina ya wenyeji Uganda ambao wamepangwa kucheza dhidi ya Ethiopia ambayo itatanguliwa na mechi baina ya Burundi na Eritrea.

Hata hivyo mechi hiyo ya Uganda dhidi ya Ethiopia iko kwenye hatihati ya kuchezwa baada ya Shirikisho la Soka Ethiopia (EFF), kuamua kutoingiza timu katika mashindano hayo kutokana na sababu za ukata.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa nchini Ethiopia (EFF) imedai kukosa fedha za kuisafirisha timu yake ya taifa hadi Uganda kushiriki mashindano hayo ambayo mwaka huu yamepangwa kushirikisha jumla ya timu 12.