Kikosi Kazi waja kivingine

Muktasari:

Kundi la Hip Hop linaloitwa Kikosi Kazi, limetoa kibao kikali kinachokwenda kwa jina la Fanya Wewe kinachotamba sokoni kwasasa, ambapo limesema huo ni mwanzo mambo makubwa yanakuja.

KUNDI la wasanii wa muziki wa Hip Hop linalojulikana kwa jina la Kikosi Kazi, limeachia kibao kipya kinachoitwa Fanya Wewe ambacho kinaonekana kutikisa kwa sasa kwenye muziki wa aina huo.

Kundi hilo linaundwa na Zaiid, Pmawenge, Nikki Mbishi, Songa, Stereo, Azma na One the Incredible ambapo wamejipanga kufanya mapinduzi ya muziki wa Hip Hop kuwa kwenye juu zaidi ya makundi mingine.

Akizungumza na Mwanaspoti Online leo Ijumaa Oktoba 9, 2020, jijini Dar es Salaam,  Zaiid amesema nyimbo hiyo imepokewa kwa kishindo na mashabiki wao, hivyo wanaamini itabadilisha upepo wa watu kupenda muziki wa aina hiyo.

Amesema awali muziki huo ulikuwa unaeleweka na wachache kutokana na kuzungumza uhalisia wa maisha ya jamii husika, bila kuweka makandokando mengi ya kuwafanya wakae tayari kusubiri kitu fulani.

"Kwasasa Hip Hop imepata mashabiki wengi, ndio maana tunajitahidi kufanya kazi nzuri  kwa kadri tuwezavyo na kundi letu lipo kwa ajili ya kuleta mapinduzi ya kuzungumza lugha ambayo itaeleweka kirahisi kwao,"

"Mwaka huu tumejipanga kutoa ngoma nyingi, lengo ni kuhakikisha muziki wa Hip Hop unakwenda juu zaidi kama ulivyo muziki laini, hilo litafanikiwa kwa asilimia 100 kwasababu tumejipanga na kuweka dhamira hiyo,"amesema Zaiid.