Kenya U-23 kuivaa Sudan

Muktasari:

  • Winga wa Vasalund ya Sweden Ovella Ochieng anatarajiwa kujiunga nayo leo mjini Khartoum akitokea Uhispania aliko na timu yake

TIMU ya Taifa ya vijana wasiozidi U-23 tayari ipo Sudan kumenyana na wenyeji kwenye mechi ya mkondo wa kwanza wa kufuzu fainali za mataifa bingwa barani kwa chipukizi hao.

Timu hiyo maarufu kama Emerging Stars, iliondoka nchini Jumapili chini ya uongozi wa Kocha wa Mathare United Francis Kimanzi. Mechi hiyo itapigwa kesho Jumatano katika Uwanja wa Khartoum huku mechi ya marudiano ikipigwa Machi 26 ugani Kasarani. Mshindi kwa ujumla wa mabao atacheza na yule baina ya Libya au Nigeria kwenye raundi ya tatu na mwisho. Kenya iliibandua nje Mauritius raundi ya kwanza kwa ujumla wa mabao 8-0.

Kwenye timu hii, winga wa Vasalund ya Sweden Ovella Ochieng anatarajiwa kujiunga nayo leo mjini Khartoum akitokea Uhispania aliko na timu yake kwa maandalizi ya kabla ya msimu. Beki Joseph Okumu wa Real Monarchs ya Marekani pia atajiunga nao kutokea huko baada ya kiungo wa FC Saburtalo ya Georgia Alwyn Tera kujiunga nao jijini Nairobi siku ya Jumamosi.