Kaze: Tumeshinda ila sijafurahishwa

Kocha Mkuu wa Yanga, Cedrick Kaze amesema licha ya kupata ushindi wa mabao 2-1 lakini timu yake haijacheza kama alivyotaka huku akiahidi kufanyia kazi suala la nyota wake kuwa na presha.

Amesema pamoja na kwamba mpango wake ulikuwa wa kuchukua pointi tatu, ila bado anayo kazi kuhakikisha timu inapokuwa inaongoza bao iweze kutulia na kwamba kufungwa pia leo imemuumiza sana huku akitamba kuwa Yanga yake ni ya mabao na soka safi.

"Leo tumeshinda ni sawa lakini sijafurahia walivyocheza vijana wangu, nimeona kuna shida ya presha tulipopata bao la pili, naenda kulifanyia kazi nachohitaji ni Yanga kushinda kila mechi na soka safi" amesema Kaze.

Kwa upande wake Kocha wa KMC, Habibu Kondo amesema hawakuwa na bahati kwani walitawala mchezo zaidi ya wapinzani na kwamba hawakati tamaa na sasa wanajiandaa na mechi nyingine inayofuata.

"Ni kweli tulianza vizuri tofauti na sasa, lakini hii ni kama Marathoni bado ni mapema na nafasi tunayo ya kurejesha kasi yetu, tunaenda kujiandaa upya na mechi inayofuata" amesema Kondo.