Kaze: Nimeona mechi nne Yanga, kazi imeisha

Mkurugenzi wa Uwekezaji wa GSM, Hersi amefichua Said kwamba juzi baada ya mchezo wa kirafiki dhidi ya Mwadui, Kaze aliwapigia simu akiwaambia amemaliza kuwasoma wachezaji wake wote.

Alisema Kaze amemaliza kazi hiyo baada ya kuwasoma mastaa 13 ambao walikuwa wanakaa benchi kwa muda tangu msimu huu uanze na tayari ameshaonyesha mambo matatu atakayoanza nayo.

“Tulidhani aliangalia mchezo wa Mwadui pekee, kumbe mwenzetu alikuwa anaangalia mechi zote nne zilizopita ikiwemo ya jana na ametueleza kila kitu kuhusu wachezaji wake wote,” alisema Hersi ambaye alionekana kushtushwa.

“Ukimsikiliza anachokueleza unaona kabisa ni kama yupo hapa, taarifa zake zina usahihi mkubwa mithili ya kocha ambaye alikuwa anafanya kazi hapa, hili limetuthibitishia kwamba huyu ni kocha sahihi kwetu.”

Hersi aliyesimamia usajili wa kikosi hicho aliongeza kuwa Kaze amekubaliana na ubora wa wachezaji, ingawa amekiri kuwa kuna madaraja tofauti ya viwango na ataanza kuwaunganisha kucheza kwa ubora.

“Anaona wapo wachezaji ambao wanahitajika kuongezewa ubora zaidi, lakini wapo ambao wataingia katika mifumo yake kwa haraka, lakini kubwa anataka kuona wanaunganika na kucheza kama timu,” alisema.

“Ametuambia hapo ndio eneo kubwa ambalo linaipa timu shida kushinda kirahisi mechi zake, ukiangalia ni kweli utaona ni jinsi gani kocha aliyepita alikuwa anapata shida kufanikisha hilo.

“Ukiondoa hilo ametaka kuwaongezea mbinu za kujua kukaba vyema na kushambulia na majukumu haya mawili amesisitiza.”