Karibu wote macho kodo kwa Pochettino

Muktasari:

Hizi hapa sehemu tano ambazo Pochettino anaweza kuibukia huko na kwenda kupiga mzigo.

LONDON, ENGLAND . SI jambo la kuficha, Mauricio Pochettino alikuwa kocha bora zaidi kuwahi kutokea Tottenham Hotspur kwa miaka ya karibuni.

Alijitolea kwa kila kitu kwenye klabu hiyo, aliwaamini wachezaji wake na alifanya kazi kwa bajeti ndogo ya usajili na bado aliifikisha timu hiyo fainali ya Ligi ya Mabingwa Ulaya.

Ni kocha mzuri, sivyo? Kwa bahati mbaya, klabu yake imemchoka na kuamua kuachana naye na kumpa kibarua hicho Jose Mourinho.

Kuna watu wanasema Spurs imefanya makosa kumwondoa Pochettino haraka, lakini wanasema hivi, kufa kufaana. Kile ambacho Spurs wamekiona cha nini, klabu nyingine zinapambana zitakipata lini na ndio maana kocha huyo Muargentina kuna kundi la timu linalohitaji saini yake. Atakwenda wapi?

Hizi hapa sehemu tano ambazo Pochettino anaweza kuibukia huko na kwenda kupiga mzigo.

1. Man United

Manchester United wamekuwa wakimtaka Pochettino tangu walipomfuta kazi Jose Mourinho, Desemba 2018. Ole Gunnar Solskjaer alitua kwenye timu hiyo kama suluhisho la muda tu kabla ya kupewa mkataba wa kudumu.

Na hiyo ni kwa sababu Pochettino ilikuwa kumpata ni lazima ulipe fidia kuvunja mkataba wake huko Spurs. Lakini, kwa sasa kocha huyo anapatikana bure na ukitazama Ole hana mwenendo mzuri kwenye kikosi cha Man United jambo linalowafanya kufikiria kwenda kumnasa mtu wao waliyekuwa wakimtaka siku nyingi. Si kitu cha kificho hata Pochettino mwenyewe hatawakataa Man United wakimtaka.

2. Arsenal

Chaguo litakalokuwa na utata. Lakini, Arsenal kwa sasa wanahitaji kurudi kwenye makali yao, hivyo hawataona hatari kumfuta kazi Unai Emery na kumpa kazi aliyekuwa kocha wa wapinzani wao, Pochettino. Msimu uliopita tu hapo, Pochettino amewaongoza Tottenham kucheza fainali ya Ligi ya Mabingwa Ulaya, huku akifuzu mfululizo michuano hiyo kwa misimu minne iliyopita. Wakati hilo likiendelea kwa Tottenham, Arsenal hao wamekuwa kwenye majanga makubwa, tangu mwaka 2016 hawajafuzu kucheza Ligi ya Mabingwa Ulaya. Bodi sasa inaweza kufumba macho na kumchukua Pochettino bila kujali ametokea Tottenham.

3. Barcelona

Pochettino ni jina la tatu kwenye orodha ya Lionel Messi ya makocha anaopenda kuwaona wakija kuinoa Barcelona. Majina mawili ya kwanza ni Marcelo Gallardo na Pep Guardiola, lakini wawili hao wote wameweka kando mpango wa kutua Nou Camp. Kutokana na hilo, Pochettino anabaki kuwa mtu pekee anayepatikana, hasa ukizingatia alishawahi kufanya kazi Hispania, alipokuwa na kikosi cha Espanyol, huyu pia ni Muargentina kama alivyo Messi. Kocha Ernesto Valverde kwa sasa yupo kwenye presha kubwa kutokana na ukweli timu imekuwa na matatizo mengi uwanjani.

4. Bayern Munich

Imeachana na kocha wake Nico Kovac na aliyekuwa msaidizi wake Hansi Flick ndiye aliyepewa majukumu ya kuwa kocha wa muda. Kwa sasa anafanya vizuri na pengine Bayern Munich inaweza kufikiria kubaki naye. Lakini, baada ya kufahamu Pochettino amefukuzwa kazi huko Tottenham, Bayern inamtazama Muargentina huyo kuwa mtu mwafaka wa kwenda kuchukua mikoba ya Kovac. Kuna nafasi ya kwenda kuchukua mikoba ya kuinoa timu hiyo huko Bundesliga.

5. Real Madrid

Ukiwa Real Madrid, unakuwa huna uhakika kama kibarua chako. Hata kama utakuwa umeiongoza kubeba mataji ya Ligi ya Mabingwa Ulaya. Lakini, ni jambo la wazi Zinedine Zidane hayupo vizuri tangu aliporudi Machi mwaka huu.Mabosi wa timu hiyo wanaweza kubadili mawazo muda wowote baada ya kuona kwamba Pochettino kupatikana tena bila ya kulipa fidia yoyote.