Kampuni ya ulinzi Hoteli aliyotekwa Mo yafunguka

Muktasari:

Mo alitwekwa Alhamisi iliyopita akiwa anaenda kufanya mazoezi kwenye Hoteli ya Colosseum na tayari familia yake imetangaza dau la Sh1 bilioni kwa mtu yeyote atakayetoa taarifa za kupatikana kwake.

Dar es Salaam/Dodoma. Ikiwa ni siku ya sita tangu kutekwa kwa mfanyabiashara maarufu nchini, Mohamed Dewji ‘Mo’ jijini Dar es Salaam, kampuni ya ulinzi ya G1, inayolinda hoteli ya Colosseum, imetoa taarifa kuhusu tukio hilo.

Askari wake ndio wanaolinda hoteli ya Colosseum ambako Mo Dewji alitekwa alfajiri ya Alhamisi iliyopita alipoenda kufanya mazoezi.

Kampuni hiyo ambayo imekuwa ikilinda Colosseum kuanzia miaka miwili iliyopita, imesema askari wake hawalindi kwa silaha za moto kwa kuwa ndio makubaliano ya mkataba na hoteli hiyo.

Uongozi wa G1 uliiambia Mwananchi jana kuwa siku ya tukio hilo Oktoba 11, walinzi watano waliokuwa zamu hawakuwa na bunduki wala bastola.

Magwila alisema kazi ya kampuni za ulinzi ni biashara na wamekuwa wakitoa nafasi kwa mteja kuchagua aina ya silaha anazohitaji zitumike kulinda kulingana na uwezo wake.

“Mteja (anapokuja) tunamwambia sisi tuna alarm, mbwa, silaha. Tunaorodhesha package tulizonazo, kwa hiyo atachagua (mteja) na hatuwezi kumlazimisha atumie silaha,” alisema Magwila.

Akizungumzia walinzi wanaoshikiliwa hadi jana, meneja rasilimali watu huyo alisema ni watano waliokuwa zamu usiku wa kuamkia Alhamisi, siku tukio lilipotokea.

“Lakini kuna wafanyakazi tofauti hapa wamekuwa wakihitajika na kuhojiwa, viongozi wa juu wameshahojiwa na polisi pia,” alisema.

Magwira alisema mkataba kati ya G1 na Colesseum hauwaruhusu kusimamia kamera za hotelini hapo.

Kuhusu daftari la kuorodhesha magari yanayoingia na kutoka, alisema utaratibu huo umekuwa ukifanyika katika malindo yao yote kwa kutumia madaftari maalumu.

Lakini alisema hilo ni tukio la kwanza kutokea katika malindo yao yote tangu walipoanza kazi miaka minne iliyopita na hawajawahi kuwa na kesi dhidi ya walinzi wake kushiriki uharifu.

Mambosasa akwama kwenda Dodoma

Sakata la kutekwa kwa Mo Dewji limesababisha kamanda wa Kanda ya Dar es Salaam, Lazaro Mambosasa na wa Kinondoni, Jumanne Murilo kushindwa kuhudhuria mafunzo ya uongozi ya makamanda wa polisi nchini yaliyofanyika mjini Dodoma.

Kamishna wa utawala na menejimenti ya raslimaliwatu wa Jeshi la Polisi, Albert Nyamuhanga alisema Kamanda wa Polisi, Simon Sirro aliagiza makamanda wote wahudhurie mafunzo hayo isipokuwa wale ambao wana kazi maalumu.

“Wale wa Dar es Salaam mnafahamu sababu iliyosababisha wasije,” alisema.