Kakolanya anawaza makubwa Simba

Muktasari:

Msimu ulioisha anakiri ulikuwa na changamoto kwake anazoamini zimemjenga na kumkomaza akili kujifunza kukabili changamoto za kazi hiyo.

KIPA mpya wa Simba, Beno Kakolanya amesema kitendo cha msimu huu kurejea uwanjani, anaamini kwake yatafunguka mambo mengi ikiwemo kupigania nafasi ya kurudi kwenye kikosi cha timu ya Taifa 'Taifa Stars'.
Simba imemsajili Kkaolonya akiwa mchezaji huru baada ya kuvunja mkataba na Yanga hivyo kuwa nje ya uwanja kwa muda mrefu kutokana na kuigomea klabu hiyo kuitumikia akishinikiza alipwe mahitaji yake ikiwemo mishahara na pesa ya usajili.
Kakolanya anasema kuna ugumu kwa mchezaji kupata madili akiwa nje ya uwanja kama anakuwa nje ya majukumu yake kwa madai soka linachezwa sehemu ya wazi anayotakiwa kuona kila mdau.
Msimu ulioisha anakiri ulikuwa na changamoto kwake anazoamini zimemjenga na kumkomaza akili kujifunza kukabili changamoto za kazi hiyo.
"Jambo kubwa ninaloshukuru Mungu ni milango ya kazi kufunguka, kuna msemo unasema mtembea bure hafanani na mkaa bure, kuwepo kazini kunanikutanisha na wadau mbalimbali wa soka.
" Sio hilo tu na ushindani wa kazi unakuwa kwenye kiwango kizuri, haitoshi kufanya mazoezi tu bila kuyafanyia kazi, hivyo kwangu nafurahia kurejea kazini.
"Kurejea kazini ni jambo lingine na ushindani wa namba kwa watu ambao nimewakuta kwenye timu pia ni hatua nyingine, unajua soka ukilala tu imekula kwako ndio maana mazoezi, nidhamu na juhudi vinatakiwa kuwa sehemu ya maisha ya mchezaji," anasema.