Kabunda ajifunga miaka mitatu KMC

Muktasari:

Kabunda alikuwa miongoni mwa wachezaji muhimu ndani ya timu hiyo akiwa kikosi cha kwanza wakati huo inafundishwa na kocha Ettiene Ndayiragije ambaye sasa ametua Azam FC.

TIMU ya KMC inaendelea na usajili kwa ajili ya msimu ujao wa Ligi Kuu Bara ikiwemo michuano ya kimataifa ambapo watashiriki Kombe la Shirikisho Afrika na leo Ijumaa wamemwongeza mkataba wa miaka mitatu kiungo wao Hassan Kabunda.
KMC wamepata nafasi ya kushiriki michuano ya kimataifa baada ya kushika nafasi ya nne msimu uliopita wa Ligi Kuu Bara ambapo Tanzania ilifikisha pointi 18, Simba ilipofanya vizuri michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika na kutolewa hatua ya robo fainali na TP Mazembe.
Kwa mujibu wa mtandao wa KMC, wamemalizana na Kabunda ambaye walimsajili akitokea Mwadui FC ya Shinyanga na hiyo ni baada ya kuonyesha kiwango kizuri.
Kabunda alikuwa miongoni mwa wachezaji muhimu ndani ya timu hiyo akiwa kikosi cha kwanza wakati huo inafundishwa na kocha Ettiene Ndayiragije ambaye sasa ametua Azam FC.
Mbali na KMC kumuongezea mkataba, saini ya Kabunda ilikuwa inawaniwa na Yanga pamoja pamoja na Azam FC.