KMC na Maguri kuna jambo

Muktasari:

  • Kocha wa timu hiyo, Etienne Ndayiragije aliliambia Mwanaspoti baada ya mchezo wao na Yanga kuwa ana kikosi kipana ndiyo maana Maguri amekosekana.


STRAIKA Elias Maguri amekosekana katika kikosi cha KMC, kwa muda mrefu sasa huku kukiwa hakuna taarifa rasmi ya kukosekana kwake.

Maguri ambaye aliwahi kuichezea Stand United, Simba na Ruvu Shooting alijiunga na KMC akitokea AS Kigali ya Rwanda ingawa hakuitumikia timu hiyo na kuamua kuvunja mkataba baada ya kushindwa kufikia makubaliano ya masilahi.

Kocha wa timu hiyo, Etienne Ndayiragije aliliambia Mwanaspoti baada ya mchezo wao na Yanga kuwa ana kikosi kipana ndiyo maana Maguri amekosekana.

“Kuna wachezaji wengi waliopo hapa, akikosekana yeye basi atacheza mwingine na yeye akiwepo basi ataonekana mwingine na timu itaendelea kuwepo,” alisema.

Alitafutwa Maguri mwenyewe ili kuzungumzia kukosekana kwake kikosini, lakini hakuwa tayari kuweka bayana zaidi ya kuomba aachwe kidogo.

Hata hivyo, Mwanaspoti lilipenyezewa mchezaji huyo alijiondoa hata kwenye kundi la mtandao wa WhatsApp la wachezaji wa KMC ambao hutumika kuwasiliana na kupokea taarifa mbalimbali kutoka kwa uongozi wa klabu hiyo.