JICHO LA MWEWE: Tanzania Covid 19 imebakia katika soka tu basi

INACHEKESHA kidogo. Sahau kuhusu matokeo ya jana Uwanja wa Taifa. Kabla ya mechi wakubwa walitangaza mashabiki 30,000 tu wangeruhusiwa kulitazama pambano la jana wakiwa uwanjani. Ni katika uwanja unaochukua mashabiki 60,000.

Kisa? Hofu ya kusambaa kwa virusi vya corona. Vinatajwa virusi hivi bado vipo na vinapatikana katika mchezo wa soka tu. Kwa nini mchezo wa soka peke yake? Huko ndio kuna punguzo la mashabiki kuingia uwanjani.

Kwingineko, Mkutano Mkuu wa CCM Dodoma hakukuwa na punguzo. Makanisani hakuna punguzo. Misikitini hakuna punguzo.

Sehemu za starehe za usiku hakuna punguzo. Kila kitu kinaendelea kama kilivyokuwa kabla ya covid na hata kwenye usafiri wa umma kwa sasa mrundikano ni kama wote tu. Kasoro soka tu.

Juzi usiku nilikuwa katika eneo la starehe linalojulikana kama ‘Kitambaa Cheupe’ pale Tabata. Idadi ya watu waliokuwepo ilikuwa kubwa, lakini zaidi hata kupishana ilikuwa vigumu. Ndicho kinachoendelea kwa sasa katika sehemu za starehe nchini. Ni katika soka ndipo tumeshuhudia uwanjani fulani ukifungiwa kwa sababu viongozi wa uwanja kutofuata masharti. Kuna wengine wamepewa onyo kali. Kinachotokea hapa tunajigeuza ndege anayeitwa mbuni. Tunachomeka kichwa katika mchanga tukijidanganya tunajificha. Eneo la mwili linakuwa wazi.

Haya mambo Rais wetu, John Pombe Magufuli aliona mbali. Hakutaka kuwa mnafiki. Baadaye hata wale waliokuwa wanataka kuitenga nchi yake nao wakafuata kile kile alichokuwa anafanya. Wakafuata njia zile zile na Rais JPM akageuka shujaa.

Kinachoendelea katika soka kwa sasa ni unafiki. Kama sio unafiki basi watendaji wanaishi katika hofu isiyojulikana. Kulikuwa na njia mbili tu za kuepuka unafiki huu. Ilipaswa kutangazwa mechi zitarudi bila ya mashabiki au zitarudi na mashabiki kwa staili ile ile waliyokuwa wanaitumia kutazama mechi kabla ya kusimamishwa.

Tangu kurudi kwa ligi mashabiki wameshindwa kufuata masharti. Kama umechunguza tabia za Watanzania ilikuwa wazi wangeshindwa kufuata masharti hayo. Kwa nini tuendelee kujidanganya na kujikosesha mapato katika mechi hii kubwa?

Mashabiki hata ukiwaingiza nusu au robo bado wanaenda kukaa pamoja. Nilikuwa natazama pambano la Namungo FC dhidi ya Sahare juzi mashabiki wa Sahare walikuwa wamejikusanya katika jukwaa la Kusini mwa Uwanja wa Mkwakwani huku maeneo mengine yote yakiwa matupu.

Mashabiki 30,000 ambao waliruhusiwa kutazama mechi ya jana nao wasingeweza kukaa mbalimbali.

Mambo mawili yalipaswa kufanywa. Hakukuwa na haja ya kuwaingiza uwanjani au kuwazuia wale wengine 30,000 ambao walipaswa kuwepo uwanjani. Rais ana baadhi ya watendaji wanafiki ambao wanaishi kwa hofu kuu dhidi yake. Kwa mfano.

Kinachoendelea kwa sasa ni hofu ya kila mmoja kujiona hawajibiki katika suala hili. Rais aliruhusu ligi zote ziendelee huku watu wakifuata masharti.

Watendaji wanashindwa kurudi kwake na kumwambia imeshindikana kuwadhibiti mashabiki. Wanachofanya kwa sasa ni kiini macho tu. Wanahofia kile kile ambacho Rais hakukihofia kwa muda mrefu sasa tangu kuanza kwa corona. Tatizo huyu anahofia atawajibishwa na yule kama atajifanya hafuati masharti. Yule anahofia atawajibishwa na mwingine wa juu yake kama akijifanya hafuati masharti. Mwisho wa Mnyororo huu unaishia kwa mheshimiwa waziri mwenyewe. Yeye labda anashindwa kurudi Ikulu na kusema imeshindikana.

Hata akisema imeshindikana nadhani Rais mwenyewe atamshangaa kwa nini amekwenda kusema kitu kilicho wazi kwake. Rais alijua isingewezekana tangu wakati ule covid 19 imepamba moto sembuse sasa inaonekana imetoweka wazi?

Tuachane na jambo hilo lililojaa unafiki mwingi ndani yake. Turudi katika maamuzi mengine kuhusu mechi ya jana. TFF ilitangaza waamuzi sita waliochezesha mechi ya Simba na Yanga. Inashangaza kidogo.

Mpaka juzi mwamuzi halisi ambaye angesimama katikati ya uwanja alikuwa anafichwafichwa mithili ya bangi. Kwa nini tumefikia huku? Tumerudi katika zama za zamani za kufichaficha majina ya waamuzi. Kwamba? Watahongwa au?

Ninachojua mwamuzi inabidi ajiandae mapema na mechi. Lakini hapo hapo tuna hofu gani wakati mechi zinaonyeshwa moja kwa moja katika televisheni. Mashabiki wa siku hizi wana faida hii. Kwa waamuzi wana hasara hii pia.

Mwamuzi akikosea uwanjani wote tunayafanyia uchambuzi makosa yake. rahisi tu. Ni kama juzi mwamuzi msaidizi, Hamis Chang’walu alikataa kwa makusudi bao la kuongoza la timu ya Sahare. Nadhani alikuwa na ajenda yake binafsi.

Baada ya mechi kuanza kuonyeshwa na Azam TV mpira umekuwa mchezo wa hadharani zaidi. Kabla hata ya vipindi vya michezo usiku watu wanatupiana katika makundi ya Whatsapp kilichokuwa kimeendelea uwanjani.

Hakuna haja ya kufichaficha waamuzi. Wakiamua kupewa pesa ni shauri yao kwa sababu mashabiki wanabakia kuwa mahakimu wazuri siku hizi.