Inter Milan waanza kumfukuzia Aubameyang kimyakimya

Muktasari:

Kwenye uhamisho wa dirisha lililopita majira ya kiangazi, straika huyo alikuwa akihusishwa na vigogo wa Hispania, Barcelona na Real Madrid, lakini sasa Inter wanaonekana kuwa siriazi kuitaka saini yake ili akajiunge na timu yao dirisha la uhamisho wa Januari litakapofunguliwa.

STRAIKA, Pierre-Emerick Aubameyang ameanza kufuatiliwa kwa karibu sana na Inter Milan wakitaka saini yake baada ya kuibuka kwa uvumi kwamba staa huyo anaweza kuachana na Arsenal dirisha la Januari.

Aubameyang kwa sasa ameanza kufikiria upya hatima yake Arsenal baada ya kuona mambo hayaendi wakiwa nyuma kwa pointi saba kuikamatia nafasi ya nne Ligi Kuu England ambayo inatoa tiketi ya kucheza Ligi ya Mabingwa Ulaya. Arsenal haijapata ushindi kwenye mechi nane mfululizo walizocheza kwenye michuano yote.

Kwenye uhamisho wa dirisha lililopita majira ya kiangazi, straika huyo alikuwa akihusishwa na vigogo wa Hispania, Barcelona na Real Madrid, lakini sasa Inter wanaonekana kuwa siriazi kuitaka saini yake ili akajiunge na timu yao dirisha la uhamisho wa Januari litakapofunguliwa.

Kocha wa Inter Milan, Antonio Conte anataka huduma ya Aubameyang dirisha hilo baada ya kuwa na wasiwasi huenda akampoteza fowadi wake Lautaro Martinez, anayesakwa kwa nguvu zote na Barcelona.