Ihefu bado hali tete

MECHI ya kwanza Ligi Kuu Bara imemalizika kwa suluhu katika Uwanja wa Sokoine, Mbeya kati ya wenyeji Ihefu waliokuwa nyumbani kucheza dhidi ya Namungo kutokea Ruangwa mkoani Lindi.

Ihefu waliongia katika mchezo huo wakiwa na kumbukumbu ya kupoteza mechi iliyopita kwa mabao 2-0 dhidi ya Azam katika Uwanja huo, wakati Namungo waliokuwa ugenini katika Uwanja wa Jamhuri Morogoro nao walipoteza kwa kufungwa bao 1-0 dhidi ya Mtibwa Sugar.

Baada ya matokeo hayo ya suluhu Ihefu watabaki nafasi ya pili kutokea mkiani wakiwa na pointi nne, wakicheza mechi nane, wameshinda moja, sare moja, wamefungwa sita, wamefunga mabao mawili na wao kufungwa 10.

Namungo wao watapanda mpaka nafasi ya nane wakiwa na pointi kumi, wamecheza mechi nane, wameshinda tatu, wametoka sare moja, wamefungwa nne, wamefunga mabao manne na wao wamefungwa matano.

Katika mechi hiyo, Namungo walionekana kupiga mashuti matano yaliyolenga lango wakati Ihefu walipiga moja, kila timu ilipiga mashuti 12 ambayo hayakulenga lango, Ihefu walipata kona 11 wakati wapinzani wao walipata 12.

Ihefu waliotea katika mashambulizi mawili kama ambavyo ilikuwa kwa Namungo ambao walimiliki mpira kwa asilimia 56, wakati wenyeji wao walimiliki kwa asilimia 44.